Nikifa msinililie, napanda meli mtumba,
Wakubwa nao wapambe, wameamua kutamba,
Kwa vipi mimi nigombe, na turufu weshalamba,
Napanda meli mtumba, nikifa msinililie!
Machozi myazuie, mkilia nitagomba,
Jeneza mlitanie, maiti mkiikomba,
Na kaburi mlichezee, wavune waliyoomba,
Napanda meli mtumba, nikifa msinililie!
Gharama msiingie, nitupeni kwenye shamba,
Au kama litokee, niwe ninacho kihamba,
Hapo mnifukie, taifa livute kamba,
Napanda meli mtumba, nikifa msinililie!
Na msinisikitikie, mviimbe vya kuimba,
Tanga msinifanyie, fedha wapeni wajomba,
Hitima msinisomee, mwenyewe nimeshaomba,
Napanda meli mtumba, nikifa msinililie!
Wanasiasa msivae, kuzika sijawaomba,
Senti msinichangie, hamna nami ujomba,
Na shangazi msilie, ni bora kuja kuimba,
Napanda meli mtumba, nikifa msinililie!
Viongozi msinisifie, wala hata kunipamba,
Mlipaswa myajue, haya yataja nikumba,
Mola awatengee, cha moto mkubwa kihamba,
Napanda meli mtumba, nikifa msinililie!
Thursday, December 1, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment