Nesi na twende sukuma, alipwe zaidi nani,
Shairi ninalituma, majibu myasaini,
Nchi naona nakama, sijui alipwa nani?
Nesi na kabebwa twende, nani alipwe zaidi ?
Makilla sina kalima, naona uhayawani,
Mla sio mkulima, ila aliye mezani,
Naamini Yakarima, hili si yake imani,
Nesi na kabebwa twende, nani alipwe zaidi ?
Hawa wanayoyasema, wanakosea anwani,
Barua yao kutuma, imekwenda ugenini,
Nchi iliyo ujima, unyonyaji mumiani,
Nesi na kabebwa twende, nani alipwe zaidi ?
Na kama ni wanachama, chama chao si makini,
Kimekufuru nasema, na wezi waweka ndani,
Mapinduzi ni lazima, au twenda kitanzini,
Nesi na kabebwa twende, nani alipwe zaidi ?
Naichelea nakama, watu hawatuamini,
Watuona ni dhuluma, tena ndugu na shetani,
Wao wazidi kuzama, sisi twajipa uzani?
Nesi na kabebwa twende, nani alipwe zaidi ?
Ninakiomba chama, kiifanye tathmini,
Nesi na tunayemtuma, mwenye thamani ni nani,
Alipwe kubwa kasma, uhai anayeghani,
Nesi na kabebwa twende, nani alipwe zaidi ?
Kubebwa wasiolima, nchi yashuka thamani,
Zimeshatota hekima, na busara mashakani,
Kama twataka uzima, haki budi kubaini,
Nesi na kabebwa twende, nani alipwe zaidi ?
Maisha sasa gharama, waumiao wa chini,
Enyi wetu waadhama, mkosacho kitu gani,
Mwala msichokichuma, hamwoni mwenda motoni?
Nesi na kabebwa twende, nani alipwe zaidi ?
Friday, December 23, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment