Monday, December 26, 2011

Viongozi ni wa nini?

Uongozi nahofia, wivi waweza ukawa,
Kama wanaojipatia, wakubwa waliokuwa,
Wanyonge kudhulumiwa, na kidogo kuchukuliwa,
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Kiongozi akipewa, milioni kwa mamia,
Na hawa nao raia, kumi hawajaijua,
Huu sio wizi hua, mchna waendelea?
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Kumi na nane saa, daktari atumia,
Wagonjwa kuhudumia, bila hata kupumua,
Twashindwa kuwaangalia, wenyewe twajiangalia?
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Nesi kote huingia, haishi kujichafua,
Matapishi hufadia, na vinyesi kuchukua,
Bungeni unayekaa, chote hicho wachukua?
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Mwalimu choki yaja, machoni na kwenye pua,
Elimu anaitoa, kesho watakaomnyonyoa,
Hili twaliangalia, tunashindwa kuamua,
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Sahani mbili mwatwaa, tonge hatujalijua,
Na kisha mwagugumia, hakiwatoshi mwaonewa,
Ibilisi mmekua, binadamu twadhania?
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Kipimo mnachotumia, mimi bado kukijua,
Kiasi gani mwatwaa, na kiasi gani mwatoa?
Nini mnakichukua, na nini mwatupatia?
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Au mwavuna mamia, hata msikopandia,
Kwingine mwakupua, vya wengine vilokua,
Hakika nawashangaa, watu msiojijua,
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Kwa haya mtachukia, ukweli nawaambia,
Mungu mkimtambua, mtageuka tabia,
Nafsi kuzizuia, wengine kuwatangulia,
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Tazameni Malaysia, zamani walipoamua,
Viongozi kukataa, malipo yaliyozidia,
Wananchi kwanza kupewa, mtaji wakaendelea,
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Kisha wao kufatia, nchi imeshanyanyuliwa,
Nyie mwanza kutwaa, nchi inadidimia,
Na Mola kawaumbua, mafuriko kutokea,
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Sasa tunawashangaa, mwashindwa wajengea,
Hivi mnategemea, muujiza kutokea,
Fisadi walizochukua, kwanini kutotumiwa,
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

Nyumba ninawaambia, kwa fakiri ndio dawa,
Hili ukishampatia, mengine atajijua,
Ila mkiliachia, dhulumati tatajua,
Viongozi ni wa nini, ustawi kama hamna?

No comments: