Thursday, August 19, 2010

Kusali si ucha Mungu

1.
Sali na kutumikiya, sala sio ubinafsi,
Sali ukiwajulia, sala sio muflisi,
Sali ukisalimia, sala sio ujasusi,
Kusali si ucha Mungu, ucha Mungu ni vitendo!
2.
Sali saa ishirini, utazipata thawabu,
Za sala kama makini, hilo halina taabu,
Binadamu ukihini, zinapungua thawabu,
Kusali si ucha Mungu, ucha Mungu ni vitendo!
3.
Kusali hii faradhi, nani asiyeijua,
Ila walio na maradhi, wataka kuhudumiwa,
Na wewe ukiwa radhi, ucha Mungu watimia,
Kusali si ucha Mungu, ucha Mungu ni vitendo!
4.
Kusali jambo la heri, shetani akukimbia,
Ila kama wewe tajiri, masikini saidia,
Na hata kama fakiri,wape wakikujia,
Kusali si ucha Mungu, ucha Mungu ni vitendo!
5.
Kusali ibada njema, mayatima bora zaidi,
Ukiwafanyia dhuluma,ibada huifaidi,
Hukusubiri kiama,ya madai na ukaidi,
Kusali si ucha Mungu, ucha Mungu ni vitendo!
6.
Ukiwanyima wajane, haki wanazostahili,
Sali ishirini na nne, sala zilizo kamili,
Hakika ni kama mavune, mtihani unshafeli,
Kusali si ucha Mungu, ucha Mungu ni vitendo!
7. .
Wazazi ukiwaasi, au kutowasaidia,
Tena na wewe mkwasi, shida hujaijua,
Sali bila wasiwasi, kitu hutoambulia,
Kusali si ucha Mungu, ucha Mungu ni vitendo!
8.
Fisadi uliyetimia, na sigda kubwa nyeusi,
Maghufira kukuombea, lazima tunajihisi,
La sivyo umeangamia,Adilizo zina nakisi,
Kusali si ucha Mungu, ucha Mungu ni vitendo!

Jini Ninayemjua

1.
Mwasema bure majini, wote mbona si wabaya,
Mnaosema pimeni, muache kuwachukiya,
Wengine wana imani, binadamu wamepwaya,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
2.
Nimfahamuye jini, hajanifanyia ubaya,
Kanishika ni mwandani,kuna mengi asaidia,
Ningekuwa mashakani,kama asingenijuwa,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
3.
Hakika anithamini, na mie namwangukiya,
Penzi lake Urulaini, kila hali katimiya,
Hunibeba usingizini, hunibeba natembeya,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
4.
Ni mwingi wa ihsani, toba tunamwangukiya,
Na masaa ishirini, kusali yake tabiya,
Uradi kwake yakini, kila pekee akiwa,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
5.
Hunipa matumaini, kila nikichanganyikiwa,
Hunionesha auni, sahili njia za kupitiya,
Na elimu kwake fani, hakuna asilojua,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
6.
Hakika ninamwamini, kwa kila analonambia,
Mengi yamo machoni, na akilini kayatiya,
La mbele hulibaini, na mie hali sijajua,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
7.
Kaniletea amani, zamani nisiyoijua,
Kaniongeza imani, kabla sikutimia,
Kaniangazia shani, awali haijatokea,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
8.
Ushairi athamini, na mengi namtungiya,
Hunisomea kitandani, mwenyewe nikajisikiya,
Na tena haya hughani, hadi nikasinzia,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
9.
Ya siri hubaini, sina nisilotambua,
Nimesinzia machoni, ila akili yajua,
Kanisihi asilani, haya kutotangazia,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
10.
Namtii mdhamini, dharau sijamfanyia,
Miaka arobaini, kwingine sijageukia,
Na dosari asilani, kwangu doa hajatiya,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
11.
Ukiniona ufukweni, basi naye naongea,
Nikiwa bustanini, upepo unatupepeya,
Na tukiwa ni majini, basi tunaogelea,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.
12.
Mshairi majinuni, moyo wake maridhia,
Ukubwa uhayawani, na heri kuzikimbia,
Malaika hawamwoni, shetani akiongea,
Jini ninayemjua, ubaya hajanifanyia.

Kaokoa mstarini

1.
Amechupia mtani, hatari kuiondoa,
Ilikuwa kimiani, ndani limeshaingia,
Kapiga abautani, mstarini kaokoa,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
2.
Beki huyu namba wani, goli hajaliachia,
Ajua wajibu nini, mwepesi kujitolea,
Uvivu ni abadani, kwake haujaingia,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
3.
Macho yake amini, kurunzi ilotimia,
Huona yote yakini, kiwanjani kitokea,
Ni mwepesi na makini, hawezi kukuachia,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
4.
Ukimkuta njiani, huwezi ukamjua,
Utadhani afkani, majinusi asojua,
Ila pale kiwanjani, ni nani wa kumvaa?
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
5.
Ni kama mashinegani, risasi anavyofyatua,
Hurudi nyuma amini, washambulizi kadhaa,
Hawathubutu kughani,shambulizi huachia,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
6.
Tumekula na yamini, kipa tutamsaidia,
Vijana wote makini, wajua pa kuanzia,
Hawapiti mstarini, chenga zitawachengua,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
7.
Mechi hii ni kuwini, kushindwa tumekataa,
Tutahaha uwanjani,hadi golini kwingia,
Nyuma ni mwiko jamani,mbele nd'o pa kuingia,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
8.
Kikosi chetu auni, aali kimetimia,
Tunataka na nishani, nchi kuitumikia,
Ni kama tupo vitani, adui hatokimbia,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
9.
Kitali hiki yakini, kama tunakirudia,
Walojifanya wahuni, mbona tulishawatoa,
Na wasiojiamini, majuzi tuliwakataa,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
10.
Anatamba kapteni, machachari alokuwa,
Azidi kujiamini,dakika zikijongea,
Tunamtia imani,kombe tunalichukua,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
11.
Makosa tumebaini, kocha anachuchua,
Na mwilini na moyoni, mbalanga zimepungua,
Anajaza akilini, ushindi kuuchukua,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!
12.
Mshairi wa kanuni, mwamini akikwambia,
Hapo ulipo chooni, shilingi waichezea,
Tokea huku uwani, mamboutajionea,
Kaokoa mstarini, nusura lingeingia!

Tikitaka

1.
Kafunga kwa tiktaka, kipa kachanganyikiwa,
Hajui lililomfika, adui ashangilia,
Nyuma akijageuka, beki mpria azoa,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
2.
Kipa hakuwa na shaka, goli halitaingia,
Lakini yamemfika, asiyoyatazamia,
Kiuno bado kashika, dunia kaichukia,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
3.
Ni goli la tiktaka, mshambulizi kaambua,
Za majeruhi dakika,ndizo zilizosalia,
Kipengo kitapigika,sekunde zikitimia,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
4.
Wachezaji waweweseka, kati hawajasogea,
Refa mwenyewe kaweka, katikati kuanzia,
Na sasa anasumbuka, wajipange kwa hatua,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
5.
Kocha tama ameshika, tumaini lapotea,
Kibarua akitaka,majani chamuotea,
Miujiza anataka,kiwanjani kutoke6a,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
6.
Filimbi imealika, mpira umezubaa,
Mwishowe wanagutuka, unaanza kutambaa,
Popote haujafika, filimbi inakataa,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
7.
Hoi hoi wanacheka, wapinzani wafurahia,
Bingwa keshafungika,tiktaka kutojua,
Mambo mchakachaka, nderemo za kushangilia,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
8.
Mmachinga tiktaka, golikipa manispaa,
Gwiji anafungika,na ushindi aotea,
Hana lililo hakika, la kufanya hajajua,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
9.
Kutenda bila fanaka, mzigo wenye balaa,
Kusoma bila kushika, huna utakalolijua,
Kufanya bila hakika, huwezi kufanikiwa,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
10.
Wenzako wanalolitaka, wewe ukalikataa,
Hukuona ni dhihaka, mbwa koko wa karaha,
Na kazi yake kubweka, mwizi humkimbia,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
11.
Uongozi wa mashaka, matatizo huyazua,
Sio wa kuaminika, matatizo kutatua,
Badala yake huruka, maji kinyesi kuvaa,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!
12.
Tafakari madaraka, si watu kunyanyapaa,
Watakiwa kuwashika, uwafae watakufaa,
Watakiwa kuwadaka, na goli halitaingia,
Ni goli la tiktaka, golikipa hajajua!

Harusi

1.
Msigeuze harusi, zikawa ni kivumbasi,
Isirafu damisi, kwa shehe na makasisi,
Mjukuu Ibilisi, kisirani na nuksi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
2.
Ndoa ibada halisi, walisema waasisi,
Jambo lataka kiasi, si kushibisha nafusi,
Haliafiki Qudusi, mwingi wa kutanafusi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
3.
Nikahi ni fahirisi, utangulizi hukisi,
Lakudumu majilisi, pasiwe na wasiwasi,
Kaskazi au kusi, vyote kupata nemsi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
4.
Ikifanywa kwayo kasi, ya riha na anisi,
Hutia doa jeusi, katika moyo mkwasi,
Na kuleta uyabisi, kila kiungo kuhisi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
5.
Harusi kama libasi, wawili ni mahsusi,
Huleta hawa fususi, ya woto na utesi,
Hawapendwi maharusi, kipendwancho ni harusi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
6.
Hili lataka kiasi, hakika si wasiwasi,
Isirafu si nemsi, muulize Abunuwasi,
Na vitabu kadurusi, uone yake nakisi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
7.
Harusi si kiharusi, jasho na wingi kamasi,
Lataka bora ususi, mambo yenu kuasisi,
Yasiyoleta nuksi, balaa nayo mikosi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
8.
Harusi kitu halisi, hakichanganywi najisi,
Haumo kwenye kamusi, uchafu nao utesi,
Vinginevyo wasiwasi, na mgeni Ibilisi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
9.
Haitaki kandarasi, kuufanya uhandisi,
Huumeza ubinafsi, jumuiya kuasisi,
Ikawa yenye wepesi, umoja na urahisi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
10.
Humkataa chunusi, anayezusha mikosi,
Huyakimbia maasi, kwa mbio zake farasi,
Ili kutunza asasi, na kumkana ibilisi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
11.
Huchongwa moja libasi, ya kukaa maharusi,
Hawa zikatanafusi, huba ikawa msosi,
Pendo kuwa ni hadithi, simulizi kila mosi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.
12.
Ila ikiwa najisi, haitokwisha mikosi,
Yatazidi na maasi, kusambaratika nafusi,
Ndoa ikawa nuksi, na familia kuhasi,
Harusi kama hadithi, huishia muflisi.

Hautonielewa

1.
Si mtu wa kudhania, wala si wa kuvamia,
Ni mpole wa tabia, na mvivu wa hatua,
Sina ninalokimbia, wala ninalokimbilia,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!

2.
Elimu yangu dunia, digrii yangu tabia,
Fikra zangu ni dua, ushauri msamaha,
Si mtu wa kulilia, wala wa kufukuzia,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
3.
Darasani nikingia, wajinga huwaondoa,
Wakabaki wanojua, toka walipozaliwa,
Neno nikilitoa, wao hulipigania,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
4.
Wazito kwenye kujua, macho yao hufumbua,
Na wale wasiosikia, mara kitu hung'amua,
Na waioona njia, tahamaki wanajua,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
5.
Kanzu niliyoivaa, kisomo imeptia,
Yajua msiyoyajua, mwilini imetulia,
Kamwe haitawaringia, wala kuwafunulia,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
6.
Masomo yangu murua, watu huchekelea,
Wengi huja kudhania, kuna kitu wameambua,
Kumbe kwao hupitia, na mbele yakaendelea,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
7.
Najua hawataelewa, hadi wanapojifia,
Kizazi kinachofatia, ndicho kitakachogundua,
Na mimi mpita njia, wajibu wangu najua,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
8.
Maswali yangu ulua, ni migodi ilojaa,
Vito vilivyochaguliwa, bora mtu kuvitwaa,
Wanaoyachanganua, thamani njema hupewa,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
9.
Mtihani wanaopewa, ni maisha kujua,
Na watu kuwaelewa, jinsi ya kuwachukulia,
Na kisha Afu kufaa, mmoya kumwabudia,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
10.
Neno langu zingatia, utu utaufikia,
Hatua zangu fwatia, njia bora utajua,
Majibu yangu tumia, yote utakujajibiwa,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
11.
Njia za mkato zafaa, kwa wale wasiojua,
Fupi refu linakuwa, na thawabu zake kujaa,
Muumba anatujua, hili halijambua,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!
12.
Beti zangu zatimia, mbele sintoendelea,
Daawa nimewapatia, yabaki kufwatilia,
Dua ninawaombea, mpate kuelekea,
Hautonielewa, tafuta 'ticha' mwingine!

Kumwoa Mzungu si Kazi

1.
Isiwe kizunguzungu, kumwoa Mzungu si kazi,
Ninawaambia wanangu,kuoa sio mapenzi,
Ila cha fedha chungu,ndio wake ufumbuzi,
Kumwoa Mzungu si kazi, kibarua kumtunza!
2.
Mzungu ataka fungu, ila sio fumanizi,
Huzipenda nyanya chungu,ila hapendi mchuzi,
Ushungi kwake ni pingu, hupenda kichwa cha wazi,
Kumwoa Mzungu si kazi, kibarua kumtunza!
3.
Hazipapatikii dengu, wala si mlaji wa nazi,
Feri kachukue changu, vibua kwake maudhi,
Hajui pikia chungu, mkaa kwake majonzi,
Kumwoa Mzungu si kazi, kibarua kumtunza!
4.
Mzungu hapendi majungu, kwa hilo nampa pengezi,
Wala hazijui kungu, kukurembulia kwa wizi,
Usimletee mkungu, kumenya ndizi hawezi,
Kumwoa Mzungu si kazi, kibarua kumtunza!
5.
Humwelewa nungunungu, ila mishale hauzi,
Huziogopa na pingu, basi usijekuwa mwizi,
Na mapanga na marungu, si Mkurya hayawezi,
Kumwoa Mzungu si kazi, kibarua kumtunza!
6.
M\zungu chake si changu, hili analimaizi,
Usifiche kwenye mvungu, atakuona jambazi,
Benki peleka mafungu, na usifanye uchuuzi,
Kumwoa Mzungu si kazi, kibarua kumtunza!
7.
Ni mtu wa wanguwangu, halitaki bumbuwazi,
Na humlipuka wengu, ukimletea uchizi,
Ama zako ama zangu, huo ndio uamuzi,
Kumwoa Mzungu si kazi, kibarua kumtunza!
8.
Wengine husema mchungu, haruhusu matumizi,
Tena hapendi ukungu, adai sana uwazi,
Ukifunika kwa mkungu, budi afanye uchunguzi,
Kumwoa Mzungu si kazi, kibarua kumtunza!
9.
Nawajuza watu Ndungu, pia na wa Mkomazi,
Mvielewe vifungu, msijeshindwa kazi,
Sio wenzetu wazungu, kuishi nao ni kazi,
Kumwoa Mzungu si kazi, kibarua kumtunza!

Pendo la binti tajiri

1.
Mimi nimelighairi, pendo la binti tajiri,
Ijapo pia mzuri, naichelea safari,
Kati isiwe ya shari, kwa joto na pia hari,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
2.
Ni Lailatkadri, sikatai fakiri,
Uzuri wake dhahiri, na mwanya ulojiri,
Macho yake ya sifuri, hupenda kuyavinjari,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
3.
Naona kama kamari, kucheza kitu hatari,
Utaisha ujibari, rijali niwe kadiri,
Nisijue adhuhuri, wala hiyo alasiri,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
4.
Nitakuwa ni kafiri, mwajiriwa si mwajiri,
Sintoiona bahari, kwa macho yenye habari,
Nitawaza nisifikiri, kutend bila hiari,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
5.
Usanii nivinjari, nikikosa kachumbari,
Kwa nje nitashamiri, ndani niwe kama ngiri,
Kitaniisha kiburi, nisiwe tena hodari,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
6.
Kuizungusha sifuri, mistari kukithiri,
Na mizani na urari, wastani usijiri,
Nitaiona fahari, lakini si shwari na heri,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
7.
Pendo la binti tajiri, mpenzi atahadhari,
Huingia taksiri, pasiwe na tena siri,
Na itazidi jeuri, uhofie yake shari,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
8.
Nimeshindwa si mahari, ila yatakayodhihiri,
Heri nibaki kafiri, hilo nilishalikiri,
Niondokane na zari, cheo na umashuhuri,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
9.
Nitamuoa fakiri, si mwana wa jemadari,
Asiye mwenye kiburi, pendo kwangu akikiri,
Tutatiana kabari, la mwili pia suduri,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
10.
Maisha yawe ya kadri, na mwendo wa tahadhari,
Tutaivuka bahari, japo papa wadhihiri,
Tutakula tafakuri, kidogo kiwe cha heri,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
11.
Tutapeana shauri, wangapi wana wajiri,
Tuwatunze kwa saburi, elimu waiabiri,
Uzeeni takbiri, waweza tupa kachori,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!
12.
Nawaasa mshairi, mwogope binti tajiri,
Labda awe dhahiri, awajali mafakiri,
Tena aso na kiburi, na mwoga kudhihiri,
Pendo la binti tajiri, mtihani niloshindwa!

Fedha Kwako Kitu Tasa

1.
Husaidiki mwanamke, fedha kwako kitu tasa,
Hupita mkondo wake, kwako kukaa hususa,
Mbegu mara zichimbuke, kuota kwako si ruksa,
Fedha kwako kitu tasa, mwanamke husaidiki.
2.
Haueleweki mwanamke, chako kisa na mkasa,
Vigumu ubadilike, ukaziona fursa,
Hayumkini ujengeke, bure mtu wajitesa,
Fedha kwako kitu tasa, mwanamke husaidiki.
3.
Labda igundulike, wewe kwa mtu asusa,
Wanaume wahongeke, jinsia iwe ngasa,
Mtu wa shika nishike, kazi kudata kipusa,
Fedha kwako kitu tasa, mwanamke husaidiki.
4
Ni ndugu wavumbulike, nao wanaokupapasa,
Au mwenzetu msagike,wazidi zimwaga posa,
Washikaji wakushike, ashikizo kuzigusa,
Fedha kwako kitu tasa, mwanamke husaidiki.
5.
Au mwenzetu mtakatike, wasaidia matasa,
Na wenye dhike mkeke, wewe huwapa mapesa,
Basi urehemeke, firdausi kugusa,
Fedha kwako kitu tasa, mwanamke husaidiki.
6.
Ungekuwa dume jike, mkwasi ungekuwa sasa,
Nyumba mwenyewe ushike,bila jicho kupepesa,
Na nduguzo wasaidike,sio kuwa kibubusa,
Fedha kwako kitu tasa, mwanamke husaidiki.
7.
Lisingelikuwa lake, gari usingelikosa,
Mtu bora maanake, kweli ungelitakasa,
Dubai nako ufike, kimataifa kuasa,
Fedha kwako kitu tasa, mwanamke husaidiki.
8.
Husaidiki mwanamke, naona bure najitesa,
Nitafute mbadalake, labda atanidodosa,
Na mimi nifurahike, mwenzi mwenye hamasa,
Fedha kwako kitu tasa, mwanamke husaidiki.

Utu si ubinadamu, wasomi watupoteza.

1.
Utu si ubinadamu, mshairi ninasema,
Utu ni jambo adimu, wengi wameshauhama,
Viumbe ni binadamu, lakini utu lawama,
Utu si ubinadamu, wasomi watupoteza.
2.
Utu si ubinadamu,itazameni kalima,
Utu ni kitu adhimu, Mola wengi kawanyima,
Utu wataka Halimu, na kubwa ndani hekima,
Utu si ubinadamu, wasomi watupoteza.
3.
Utu ya juu nidhamu, utadhani ni karama,
Utu ya haki hukumu,bila kugwaya uhasama,
Utu adili nadhimu, uadiifu wa dawama,
Utu si ubinadamu, wasomi watupoteza.
4.
Utu ni kutakadamu, mwenendo na tabia njema,
Utu ni uislamu, fundisho mpaka kiyama,
Sio wote wanadamu, utu wapewa heshima,
Utu si ubinadamu, wasomi watupoteza.
5.
Wapo vinara hakimu, viongozi wa heshima,
Kadhalika wanajimu, nyota waliozisoma,
Ila utu madhulumu, hawana cha chini kima,
Utu si ubinadamu, wasomi watupoteza.
6.
Wapo mashehe na walimu, na mapadri waadhama,
Jichoni ni binadamu, kubwa twawapa heshima,
ila nakisi yadumu, utu kwao umehama,
Utu si ubinadamu, wasomi watupoteza.
7.
Twawaona binadamu, utu vipofu nasema,
Utu sio la ghanimu, wala kwa cheo kuvuma,
Maskini huwa rahimu, malaika kumpema,
Utu si ubinadamu, wasomi watupoteza.
8.
Mtoto huufahamu, mkubwa kutokuusoma,
Mjinga huwa karimu, mwenye akili kuzama,
Nisai huwa hirimu, rijali akachutama,
Utu si ubinadamu, wasomi watupoteza.

Kiumbe kweli kijembe

1.
Kiumbe kweli kijembe, na wengine kama wembe,
Hawana lililo na chembe, ya tosheko wasigombe,
Hata vipi umpambe, lazima tope arambe,
Kiumbe kweli kijembe, japo kakosa mapembe!
2.
Mpambe mwana kijembe, na jambo nambe msambe,
Ni jipu lenye uvimbe, maumivu usiombe,
Kikwepe hicho kikombe, ni shubiri usiilambe,
Kiumbe kweli kijembe, japo kakosa mapembe!
3.
Ni mende mwenye uzembe, hata kwa vipi atambe,
Mwache kote ajigambe, mchana shida aimbe,
Mngoje Kigurunyembe,upuuzi wake ujumbe,
Kiumbe kweli kijembe, japo kakosa mapembe!
4.
Kiumbe sio mzembe, ila mwingi wa vijembe,
Msanii umuimbe, si mtamba sio tembe,
Usimuone ni ng'ombe, ana lake aliombe,
Kiumbe kweli kijembe, japo kakosa mapembe!
5.
Ni vigumu asigombe, akidai hata chembe,
Lake hutaka litambe, la kwako huona mwembe,
Kwa maslahi mpambe, ila kuzalisha mbembe,
Kiumbe kweli kijembe, japo kakosa mapembe!
6.
Na mikwara aichimbe, na fadhila azikombe,
Msambe nisambe kumbe, \snukrani usilambe,
Mja kachukue jembe, waachie ndugu wagombe,
Kiumbe kweli kijembe, japo kakosa mapembe!

Mswahili yeye ngono

1.
Tumeshasemwa weusi, na dunia yamaizi,
Ngono kwetu sarakasi,kuiacha hatuwezi,
Nyuma hufata mikosi,dhuluma na ugandamizi,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
2.
Mswahili yeye ngono, vinginevyo haviwezi,
Ona wakata viuno,walio nao ujuzi,
Hapanayo mabishano,Afrika huwawezi,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
3.
Ni asilimia tano,ndiyo ina uongozi
Baki tisini na tano,ni ya pombe na mapenzi,
Ni yanini maulizano,nchi hatuendelezi?
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
4.
Mswahili mke, mme, wote watazama chini,
Na sifa ya mwanamme,wangapi anadhamini,
Bora mema wayahame, jinsi wanavyoithamini,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
5.
Mengine hafikirii, kwa muda unaofaa,
Elimu hakimbilii, ila ngono ikitoa,
Na cheo hakichukui, ila ashiki kuvaa,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
6.
Heri wakuu wa kale,hili sana walijua,
Kuhasi wachagulile,ili tija kunyanyua,
Tufanyeje wateule,nchi yetu kuifaa?
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
7.
Mwili ni yetu dunia, nyingine hatuijui,
Mijitu mvi yajaa,bado hawayakinai,
Vitanda vinazagaa,hadi ofisi zadai,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
8.
Akikwaa utajiri, ngono ndiyo namba wani,
Hatendi kwa watu kheri, ila apate hisani,
Wanaponza itihari, nyoyo hazina imani,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
9.
Na cheo akikikwea, ngono ni yake shabaha,
Chupi atakazovua, hesabu hutoijua,
Ofisi alimokua,danguro Selemania,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
10.
Ukweli hawaupendi, sikia wanavyolalama,
Mwaukataa ufundi,hali mwavifua vyuma?
Nenda China na Uhindi,uone walivyo salama,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
11.
Mawaziri wanakaa, vibinti kuvitumia,
Milioni watumia,raha kujinunulia,
Nchi yateketea,hakuna anayejua,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
12.
Mkiwapa misaada, vibaya wanaitumia,
Waanza fuga vimada,ndani yote Tanzania,
Siasa sasa mnada,na ngono yasaidia,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
13.
Kichefuchefu chafua, wataka hutaki chukua,
Rohoni asiyejijua,Uongozi hufulia,
Tamaa wanaojaa,huishi wafu wakiwa,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.
14.
Hili nalishuhudia, japo nitajachukiwa,
Mola ninamlilia, denda miye kunivua,
Watu nikawatumikiya, hadi siku ya kujifia,
Mswahili yeye ngono, uongozi hauwezi.

Kismati mara moja,

1.
Ukibahatika tena, kaushukuru mkaja,
La leo sio la jana, na wala hili si kioja,
Na kuja ni kujaana, kupishana si useja,
Kismati mara moja, mwaka ujao kiroja!
2.
Kipofu mwezi kuona, kachelewa jenga hoja,
Na sasa giza aona, Han teja wala tija,
Huona asichoona, na kusifu lisokuja,
Kismati mara moja, mwaka ujao kiroja!
3.
Mtu kama akili hana, hudharau lenye tija,
Akasifu liso maana, hata hekima kufuja,
Pepoze sio mwanana, Ni mtu wa kwenda na kuja,
Kismati mara moja, mwaka ujao kiroja!
4.
Hajengi lenye maana, wala hatimizi haja,
Huona walo mabwana, na kujifanya yeye mteja,
Haukatai utwana,ili awe na mirija,
Kismati mara moja,mwaka ujao kiroja!
5.
Kismati hutoona, kikikujia mara moja,
Yako hayawezi fana, bahati haitokungoja,
Mtazidi kupishana, na wa juu chini kuja,
Kismati mara moja, mwaka ujao kiroja!
6.
Mambo mchana kusana, hata za juja na majuja,
Ustawi mwana sana, uvivu hauna tija,
Neema kama hazina, kutunzwa jambo la haja,
Kismati mara moja, mwaka ujao kiroja!
7.
Kismati sintokana, hili kiungo daraja,
Ni kukosa na kufana, kuvua na kuvaa koja,
Kiumbe aso mtwana, hajifunzi kwa lahaja,
Kismati mara moja, mwaka ujao kiroja!
8.
Kismati muamana, huja hakiwindwi mja,
Ila yataka amana, pale kwako kitapokuja,
kushika ukikiona, tena sio kwa rejareja
Kismati mara moja, mwaka ujao kiroja!

Raha iko ndani yangu

1.
Sishughulishwi na ya nje, raha iko ndani yangu,
Ni vioja vilioje, kuwatazama wenzangu,
Hujiluliza wafanyaje, wawe kama watu-mungu,
Raha iko ndani yangu, sishughulishwi na ya nje.

2.
Wajua Kilwa Kivinje, hii si fatwa yangu,
Kila kitu mkivunje, nachieni nafsi yangu,
Makamu haya si njenje, kutibwirika si yangu,
Raha iko ndani yangu, sishughulishwi na ya nje.

3.
Raha iliyo kwa nje, kwangu mawingu na mbingu,
Siipati hata punje, na haipoozi moyo wangu,
Ila ndani niikunje, huona uzima wangu,
Raha iko ndani yangu, sishughulishwi na ya nje.
4.
Napenda walio nje, ila sio raha yangu,
Hili sio kitu uonje, ila tanafusi kwaangu,
Ni fikra zilo fiche, ndani mawazo yangu,
Raha iko ndani yangu, sishughulishwi na ya nje.
5.
Sishughulishwi na ya nje, furaha i ndani yangu,
Maisha msinipunje, Tao ni mwalimu wangu,
Na njia msiikunje, zipite hatua zangu,
Raha iko ndani yangu, sishughulishwi na ya nje.
6.
Hayaniwasi ya nje, si ya Mchina si Mzungu,
Weshaniita Machenje, naujua utu wangu,
Hata viungo mvunje, kuruka ni haki yangu,
Raha iko ndani yangu, sishughulishwi na ya nje.
7.
Nakera walio nje, hawaingii ndani yangu,
Huku na huko wahanje, hawaoni langu fungu,
Waache hao wabanje, mafua sio machungu,
Raha iko ndani yangu, sishughulishwi na ya nje.
8.
Nawaachia nyie ya nje, ya ndani ni haki yangu,
Siidai hata punje, kuleni yote mafungu,
Ila ya ndani msionje, ya kwenye wangu uvungu,
Raha iko ndani yangu, sishughulishwi na ya nje.

Kisima chenu cha fikra

1.
Mnaopenda vya bure, anzeni kushangilia,
Haya hapa ya bwerere, ruksa kuvichukua,
Wanayaweza ngedere, kwenu halitowastua,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
2.
Sio Wachagga si Wapare, miteremko mwatumia,
Si Wamasai si Wakwere, vya bure waporomoshewa,
Yanini kiherehere, malipo kutarajia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
3.
Zimejaa ni bwerere, msiache kukimbilia,
Pasina kiherehere, ndoo tieni na kutoa,
Mhifadhi na mchore, akilini kuzitia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

4.
Ila vichwa msifure, hamjui msojua,
Bunduki sio gobore, mwaweza kujilipua,
Na Dar sio Harare, udikteta si tabia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
5.
Ninamuenzi Nyerere, akili alitumia,
Afrika nani sare, na yeye kulingania?
Vipi fikra tugure, bila kuzifikiria,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

6.
Viazi sio vibere, ladha ukijagundua,
Uhuni sio ukware, fumanizi likiuumbua,
Cha kulipa si cha bure, hasara hutoijua,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

7.
Fikiri ndio kusare, lugha ukishaijua,
Naihofia Lahore, japo mie Mtanzania,
Mengine yote wapore, ila fikra mtaumia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
8.
Kazi mbaya si kazi bure, usia ninautoa,
Maradhi kama ni ndere, mbwani chozi kukufichua?
Ushirikina si gere, ila kuuza ubaya,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

Kisima chenu cha fikra

1.
Mnaopenda vya bure, anzeni kushangilia,
Haya hapa ya bwerere, ruksa kuvichukua,
Wanayaweza ngedere, kwenu halitowastua,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
2.
Sio Wachagga si Wapare, miteremko mwatumia,
Si Wamasai si Wakwere, vya bure waporomoshewa,
Yanini kiherehere, malipo kutarajia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
3.
Zimejaa ni bwerere, msiache kukimbilia,
Pasina kiherehere, ndoo tieni na kutoa,
Mhifadhi na mchore, akilini kuzitia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

4.
Ila vichwa msifure, hamjui msojua,
Bunduki sio gobore, mwaweza kujilipua,
Na Dar sio Harare, udikteta si tabia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
5.
Ninamuenzi Nyerere, akili alitumia,
Afrika nani sare, na yeye kulingania?
Vipi fikra tugure, bila kuzifikiria,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

6.
Viazi sio vibere, ladha ukijagundua,
Uhuni sio ukware, fumanizi likiuumbua,
Cha kulipa si cha bure, hasara hutoijua,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

7.
Fikiri ndio kusare, lugha ukishaijua,
Naihofia Lahore, japo mie Mtanzania,
Mengine yote wapore, ila fikra mtaumia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
8.
Kazi mbaya si kazi bure, usia ninautoa,
Maradhi kama ni ndere, mbwani chozi kukufichua?
Ushirikina si gere, ila kuuza ubaya,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

Kisima chenu cha fikra

1.
Mnaopenda vya bure, anzeni kushangilia,
Haya hapa ya bwerere, ruksa kuvichukua,
Wanayaweza ngedere, kwenu halitowastua,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
2.
Sio Wachagga si Wapare, miteremko mwatumia,
Si Wamasai si Wakwere, vya bure waporomoshewa,
Yanini kiherehere, malipo kutarajia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
3.
Zimejaa ni bwerere, msiache kukimbilia,
Pasina kiherehere, ndoo tieni na kutoa,
Mhifadhi na mchore, akilini kuzitia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

4.
Ila vichwa msifure, hamjui msojua,
Bunduki sio gobore, mwaweza kujilipua,
Na Dar sio Harare, udikteta si tabia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
5.
Ninamuenzi Nyerere, akili alitumia,
Afrika nani sare, na yeye kulingania?
Vipi fikra tugure, bila kuzifikiria,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

6.
Viazi sio vibere, ladha ukijagundua,
Uhuni sio ukware, fumanizi likiuumbua,
Cha kulipa si cha bure, hasara hutoijua,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

7.
Fikiri ndio kusare, lugha ukishaijua,
Naihofia Lahore, japo mie Mtanzania,
Mengine yote wapore, ila fikra mtaumia,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!
8.
Kazi mbaya si kazi bure, usia ninautoa,
Maradhi kama ni ndere, mbwani chozi kukufichua?
Ushirikina si gere, ila kuuza ubaya,
Kisima chenu cha fikra, choteni, kunyweni mtosheke!

Taifa la wachuuzi

1.
Kunayo moja tu kazi, nayo si uzalishaji,
Ni tarafu ya uchuuzi, kila kijiji na kila mji,
Hatima yake ajizi, naona bora nihoji,
Taifa la wachuuzi, laweza kuendelea?
2.
Taifa la wachuuzi, bila ya wazalishaji,
Hata kwa chipsi viazi, Iwe nje uagizaji,
Naamini haliwezi, kuyakidhi mahitaji,
Taifa la wachuuzi, laweza kuendelea?
3.
Uchuuzi hauongezi, wala kupanua mtaji,
Kaziye ni matembezi, maikro kuifariji,
Kama wataka makuzi, lazima uzalishaji,
Taifa la wachuuzi, laweza kuendelea?
4.
Nchi yataka majazi, daraja walizo magwiji,
Bila kuifanya kazi, bidhaa kuzitaraji,
Kwenda mbele hatuwezi, tutabaki wafujaji,
Taifa la wachuuzi, laweza kuendelea?
5.
Taifa la wanunuzi, tena bila wauzaji,
NI taifa angamizi, liso usasahishaji,
Duni wake viongozi, hawafai kutaraji,
Taifa la wachuuzi, laweza kuendelea?
6.
Sio nchi ilo azizi, ya wageni kuja hiji,
Si pahala pa uzuzi, jipya kamwe haliji,
Ni mahala pa wakwezi, wakulima na walaji,
Taifa la wachuuzi, laweza kuendelea?
7.
Nchi yataka darizi, malengo na upangaji,
Watu wataka malezi, na kuengwa makuaji,
Ardhi yataka wekezi, udumu uzalishaji,
Taifa la wachuuzi, laweza kuendelea?

8.
Sasa yetu kubwa kazi, tuubebe uzalishaji,
Tufanye maamuzi, kwenye miji na vijiji,
Kisha tuanze kazi, Kukidhi yetu mahitaji,
Taifa la wachuuzi, laweza kuendelea?

Diwani fungua macho

1.
Waweza boresha kata, si kama ilivyokua,
Yaweza isha matata, kata ikajitanua,
Wawza maliza ukata, kampuni mkikwaa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
2.
Diwani ni kama nta, umoja ukatokea,
Hamasisha wana kata, vikao wapate kaa,
Maamuzi kuyakata, mengi yenye manufaa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
3.
Maendeleo ni vita, katika yetu dunia,
La sivyo mtapakata, umaskini sawia,
Neema hamtoipata, hadi mwisho wa dunia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
4.
Kata lazima kuota, ndoto zenye majaliwa,
Msikubali kusota, wengine wanakimbia,
Boresheni Mkukuta, muweze kuja kupaa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
5.
Wenngine wanawasuta, na pia kuwanyanyapaa,
Neema hamjatafuta, vijiweni mnakaa,
Za mchana mnaota, ndoto zisizowafaa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
6.
Fikra hamjapepeta, rai kuzichanganua,
Yapo mambo mia sita, chache mwaweza chagua,
Na hapo mkajikita, mazuri kukokotoa,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
7.
Ubinafsi wawasuta, madalali wa mitaa,
Mwauza hata viota, wapi ndege watakaa?
Historia mtadata, itawachora vibaya,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
8.
Diwani acha kuteta, neema budi kuzua,
Na wala usije ota, utakuja kuizoa,
Haipati maji kata, bila mtungini kwingia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
9.
Usiwe wa kupitapita, majilisi hujakaa,
Wakazi nao kuteta, ndio njia ya kuanzia,
Mawazo mkayavuta, matatizo kugundua,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
10.
Ufumbuzi kutafuta, kero zilizoenea,
Diwani kavae ngata, mtungi kichwani tia,
Na kama kucheza kwata, gwardi kuparamia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
11.
Diwani usiwe mtata, mtu wa watu jua,
Madhambi yote kufuta, wewe yakutegemea,
Itakate yenu kata, ing'are kuliko sinia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
12.
Diwani rai tafuta, na elimu kimbilia,
Usijefanye dokata, la saba halijatimia,
Watakuona kiputa, nundu kuja kukulemea,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!
13.
Natupa yangu karata, geresha halijanifaa,
Ukiona unatota, bafuni hujainigia,
Basi tambua mafuta, mwilini yamezidia,
Diwani fungua macho,waweza boresha kata!

Mbunge jimbo ni lako

1.
Mbunge umepotea, mwenzetu hatukuoni,
Siku tulipokuchagua, ulitupa nyingi imani,
Wewe kukutegemea, kutuondoa mashakani,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
2.
Mwisho kututembelea, hatukumbuki ni lini,
Ahadi ukazitoa,zote kwishia mitini,
Kinyongo chaning'inia,nyongo watu tumbueni,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
3.
Habari zimeenea, waishi ughaibuni,
Umukua milionea, tena wa matrilioni,
Umaskini wachukia, utakutumbua ini,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
4.
Hewa utakuchafulia, wanuka umasikini,
Huwezi kuvumilia, kuona waso thamani,
Na waziri umekua, sikuzote safarini,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
5.
Hakuna tulilopangua, mipango hukubaini,
Halipo lililopotea, kwetu hukuwa na thamani,
Hapana kilichochipua, vilifia ardhini,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
6.
Hapo ndipo pa kuanzia, kisha tufike mwishoni,
Tulikupa twachukua, wangung'unika nini ?
Vipi utamwamkua,asiye mwako machoni ?
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
7.
Wananchi watachukua, kilicho mwako mkononi,
Na hili sintowaambia, sioni lina walakini,
Kichochoro 'kitumia, kumejaa barabarani,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
8.
Mvuvi anapovua, samaki huwa kapuni,
Wewe umeshakwapua, vyako viko makwapani,
Usiotee kurejea, hiyo ndoto ya mbeleni,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
9.
Wazee mmeshupaa, mmetufanyia nini,
Magenge mmeyazua,kung'atuka mwahaini,
Juu tutawasanzua,vijana fursa wapeni,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
10.
Wanawake wameamua, kazi kuja waonyesheni,
Haraka pisheni njia, midume msio makini,
Nchi twataka komboa, umalizike uzaini,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!
11.
Vijana wameamua, kuingia madarakani,
Filamu kutuchezea, si ile ya umaskini,
Ya kuukata kwa sanaa, tushangaze duniani,
Mbunge jimbo ni letu, usije ukaturusha!

Mkuu wa wilaya mambo ?

1.
Wilaya inaugua, hili ndugu walijua,
Tabibu anatakiwa, wilaya kupata dawa,
Wote mnajifungia, ofisini mnasinzia,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
2.
Maendeleo vitendo, lazima kuyapangia,
Mengine wekeni kando, kwanza muonyeshe njia,
Hayo mawazo ya mgando, zamani tumeshakataa,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
3.
Wilaya ina ardhi, tupange cha kuzalisha,
Na jinsi ya kuhifadhi, tija tukaizungusha,
Wilaya ipande hadhi, na kujitofautisha,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
4.
Wilaya ina madini, vipi lije tumaini,
Utoke umaskini, watu kukosa thamani,
Tuipate afuteni, vijijini na mjini,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
5.
Wilaya ina maziwa, vipi tuyapate maji,
Ili yaweze kutumiwa, na kuwa ni wetu mtaji,
Mashamba kunyeshea, tukafanya uvunaji,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
6.
Wilaya ina mifugo, tuwafuge namna gani,
Wasiwe kwetu mzigo, bali amana makini,
Na sisi tuwe vigogo, Mbeya na umasaini,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
7.
Wilaya ina asali, vipi mbaya yetu hali,
Tunazo na pilipili, mbona maisha shubili,
Twala na kusaza wali, ila hatuna afadhali,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
8.
Nini chanzo cha tatizo, lazima tupate jua,
Utafiti mzomzo, lazima kujifanyia,
Tupate maelekezo, njia ipi kutumia,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
9.
Wengi wasema nchini, sisi mbona matajiri,
Hatunao tu umakini, ndio twawa mafakiri,
Ili tuwe sio duni, tuianze mpya ari,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
10.
Wilaya sio ngomani, wilaya ni kampuni,
Meneja watafuteni, miradi waje baini,
Mipango nayo wabuni, kwa mkubwa umakini,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
11.
Wialay ni kampuni, viranja badilikeni,
Urari uwe juani,wala sio mafichoni,
Nini wilaya thamani, na wapi mlipo duni,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
12.
Amali zenu jueni, hizo ni hisa yakini,
Watu waelimisheni, kwa KIswahili laini,
Wasoenda darasani, nao pia watamani,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
13.
Ukuu sio masuti, wala fashioni mpya,
Huo ni uzumbukuti, mafiga hayana chafya,
Wananchi ndio yakuti, wataka moyo kulea,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?
14.
Ukubwa sio ofisi, fenicha nalo gari,
Ukuu si kutanafusi, wala njaa ya fahari,
Uongozi uasisi, heri ya wote si shari,
Mkuu wa wilaya mambo, au yote kwako sawa ?

Mkuu wa mkoa vipi ?

1.
Kiongozi kazi yake, kutatua matatizo,
Ukijenga uezeke, tena utumie nguzo,
Madaraka usishike, kama fikra hamnazo,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
2.
Au huoni tatizo, wakati yakuzunguka,
Ofisi ni kipoozo, toka nje kugutuka,
Teremka ngazi hizo, hadi chini ukafika,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
3.
Wewe Waziri mkuu, mkoa yako milki,
Acha tu ya kunukuu, ingia katika mikiki,
Silaha yako mguu, kwalo haudanganyiki,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
4.
Wewe mkubwa gavana, milioni wako chini,
Hili na lile hawana, wakungoja mitaani,
Hatua iwe amana, njoo nawe mstarini,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
5.
Mkuu onyesha njia, watu wataifuata,
Ikiwa wanapotea, basi wewe ni matata,
Panga kisha kupangua, hatuutaki ukata,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
6.
Jamii iwe na nyumba, wameyachoka manyatta,
Pambanueni vihamba,watu wapate karata,
Siasa zile za kuimba,hazina wa kufuata,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
7.
Barabara kazi yako, zijengwe ima fa ima,
Juu wako nyuma yako, wewe sema waja hima,
Wala msikae kitako, hadi iishe zahama,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
8.
Miradi anzisheni, kama vile kampuni,
Watu wajumuisheni, hisa ziwe maishani,
Na pasiwe na utani, lazima mle yamini,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
9.
Miundombinu anzeni, juu nao wamalize,
Kusubiriana acheni, wenyewe sasa mjikaze,
China kajifunzeni, wanavyofanya seuze,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
10.
Juzi wamejenga treni, iendayo sana kasi,
Wameiga kwa Wajapani, ufundi pia asasi,
Kama vile ni utani, safari zao fususi,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
11.
Nendeni India muone, watengeza kila kitu,
Ni mikoa ya wajane, walakini watukutu,
Wanakua mara nane, sisi kwao hatufutu,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?
12.
Paeni nako Brazili, mashine wakokotoa,
Kila kitu ni sahili, wazalisha kwa mamia,
Hawanao ujahili, milango wamefungua,
Mkuu wa mkoa vipi, au huoni tatizo?

Mashairi yanasema

1.
Mashairi yanasema, mengi yanatuambia,
Kwa watu wenye hekima, kauli huzizingatia,
Na palipo waadhama, waidha huzingatia,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
2.
Yashangaza hizi zama, kuipuuza sanaa,
Zunguka nchi nzima, ushairi unapwaya,
Nai zinazorindima, adili zadidimia,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
3.
Shuleni wameshakwama, nani kutunga ajua,
Afundishaye ni ndama, ng'ombe wameshapotea,
Kukamua wamekwama, upepo wawapepea,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
4.
Redioni wamehama, watunzi waliokua,
Sasa zimebaki ngoma, na makelele kufua,
Halfani hana hema, baridi augulia,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
5.
Andanenga kasimama, gumzoni kaingia,
Utunzi kaona noma, maslahi yasinyaa,
Wala hapana heshima, wala wa kutuangalia,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
6.
Ninatweta, ninahema, hili sikulitegemea,
Nchi yenye takrima, utunzi isiyowafaa,
Watu wafunga kalima, busara kuyoyomea?
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
7.
Kitu gani anasema, Shaaban alipokua,
Mnyampala muadhama, hili hakulifikiria,
Shehe Abedi daima, asingelitegemea,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
8.
Mochiwa kabaki nyuma, hadi anajiondokea,
Mla mbovu kainama, hili hakulisikia,
Abdulatifu kahama, Uingereza kaselea,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
9.
Kiswahili kitazama, bila utunzi kukua,
Wasiokitakia mema, hawataki kukitumia,
Vyuoni wanakilima, eti sio maridhia,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
10.
Elimu imesimama, tena yazidi sinyaa,
Kiswahili kukinyima, ruksa kufundishia,
Ni kweli mkataa pema, panakomwita pabaya,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
11.
Mitume wametuhama, lugha yetu kuiua,
Tambiko zimegangama, hakuna wa kutusikia,
Na midomo imeachama, twadhani twaomba dua,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
12.
Mushawari kagoma, uzuri umepotea,
Sasa twaicheza ngoma, asili tusioijua,
Akili zimetuhama, tumebaki kubabia,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
13.
Mashairi yanasema, viziwi watasikia,
Makilla akilalama, wengi watamsaidia,
Ni tamu lugha ya mama, utumwa nyingine kua,
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!
14.
Semeni mliosoma, Mlokozi chokonoa,
Kahigi tia kalima,na vijana mlioingia,
Nchi yataka neema, ije vipi bila lugha?
Mashairi yanasema, asosikia kiziwi!