Sunday, September 25, 2011

Mimi kwako ni mnyonge.

Mimi kwako ni mnyonge, ukipanda nnashuka,
Hakika mimi ni bwege, rahisi kudanganyika,
Isitoshe ni kikongwe, siwezi vita kutaka,
Hakika mimi mnyonge, salama yangu Rabuka!

Kwanini bure niringe, na huu wangu mzuka,
Si polio nijikinge, mama asipokumbuka,
Si ukimwi wanitenge, wasotaka kuumbuka,
Hakika mimi mnyonge, salama yangu Rabuka!

Si ugonjwa niugange, nisije kutaabika,
Hili ni la kwangu singe, kwalo nimebahatika,
Haiwezekani nivunge, fungate ilokamilika,
Hakika mimi mnyonge, salama yangu Rabuka!

Mjeshi naye achunge, na staha si hulka,
Kwa Mhehe ajinyonge, maudhi yakishindika,
Wenye kusepa wapange, kabla kuharibika,
Hakika mimi mnyonge, salama yangu Rabuka!

Mimi ni mnyonge, kushindwa nimeshindika,
Ila yangu niyalenge, sina la kubabaika,
Waache nje waringe, ya ndani ninayashika,
Hakika mimi mnyonge, salama yangu Rabuka!

Sina gele kwa wabunge, wala waliostahika,
Na matajiri nipunge, siwezi kukubalika,
Nawatafuta wanyonge, moyo wanaolainika,
Hakika mimi mnyonge, salama yangu Rabuka!

Sina jeuri ya kenge, kwa kuwa mamba ni kaka,
Siigizi ya madenge, ya kwangu yakishindka,
Kwa watu siombi tonge, kulala njaa naridhika,
Hakika mimi mnyonge, salama yangu Rabuka!

Wacha mizinga wachonge, shambani kuitundika,
Chora watupe vidonge,kisha vaja haribika,
Ona mbegu wazitwange, wakaja kuhamanika,
Hakika mimi mnyonge, salama yangu Rabuka!

Ya Ghaniyu unichunge, nisiwe wa kuropoka,
Miguu yangu ifunge, kwenye shari kutofika,
Na mkono uniunge, kwenye wema kuendeka,
Hakika mimi mnyonge, salama yangu Rabuka!

Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Chama changu kinatamba, kufanya liso jipya,
Chataka kujivua gamba, si kuzaliwa upya,
Ni wimbo wanaoimba,bila ya dira kuijua,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?


Hawezi zaa mgumba, vipi wamtumainia,
Shahada hakiwi gumba, vipi utashahadia,
Taarabu sio rumba, huko si kutuharibia?
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Usiku hucha kwa komba, gizani nyendo ajua,
Riziki atazikomba, ghalani akazitia,
Utakuwa ni mshamba, ukija mwigilizia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Sio hai lako gamba, mara linshapwelelea,
Kwenye mizani ja pamba, hadhi yako inshakua,
Wazeeka wajiremba, nguchuro watahofia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Chama hakijawa gumba, hakijakoma kuzaa,
Vijana wanakipamba, wakosaje kukiinua?
Wazee kaeni chemba,umri umewazidia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Hakuna wa kumchimba, ni ukweli tunatoa,
Limechachamaa dimba, soka litatuengua,
Rijali tusipoomba, mechini kuja ingia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Kufumbua na kufumba, hatimaye kufungua,
Kalenda ya Muumba, haina wa kungojea,
Mwokozi kitindamimba, mziwanda hatofaa,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Wewe wajivua gamba, badala kizazi kpya?
Ah, shangazi na wajomba,hamjioni mwaishia?
Kompyuta zawagomba,'facebook' yawazingua?
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Kashfa mnaziomba, na wengine kuzomea,
Siasa hizo za mtamba,fahali akimkataa,
Ubunfifu na ugumba,ni nani atavioa?
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Na dini mnaziomba,siasa kuwasaidia,
Huku wimbo mnaimba,udini unaingia?
Njaa yaua wajomba,hata makombo watwaa?
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Mahakama sasa jumba, siasa kuzikamia,
Polisi na jambajamba, chama kukisaidia,
Tunaitafuta kamba,kunyonga demokrasia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Wednesday, September 21, 2011

Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Chama changu kinatamba, kufanya liso jipya,
Chataka kujivua gamba, si kuzaliwa upya,
Ni wimbo wanaoimba,bila ya dira kuijua,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Hawezi zaa mgumba, vipi wamtumainia,
Shahada hakiwi gumba, vipi utashahadia,
Taarabu sio rumba, huko si kutuharibia?
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Usiku hucha kwa komba, gizani nyendo ajua,
Riziki atazikomba, ghalani akazitia,
Utakuwa ni mshamba, ukija mwigilizia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Sio hai lako gamba, mara linshapwelelea,
Kwenye mizani ja pamba, hadhi yako inshakua,
Wazeeka wajiremba, nguchuro watahofia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Chama hakijawa gumba, hakijakoma kuzaa,
Vijana wanakipamba, wakosaje kukiinua?
Wazee kaeni chemba,umri umewazidia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Hakuna wa kumchimba, ni ukweli tunatoa,
Limechachamaa dimba, soka litatuengua,
Rijali tusipoomba, mechini kuja ingia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Kufumbua na kufumba, hatimaye kufungua,
Kalenda ya Muumba, haina wa kungojea,
Mwokozi kitindamimba, mziwanda hatofaa,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Wewe wajivua gamba, badala kizazi kpya?
Ah, shangazi na wajomba,hamjioni mwaishia?
Kompyuta zawagomba,'facebook' yawazingua?
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Kashfa mnaziomba, na wengine kuzomea,
Siasa hizo za mtamba,fahali akimkataa,
Ubunfifu na ugumba,ni nani atavioa?
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Na dini mnaziomba,siasa kuwasaidia,
Huku wimbo mnaimba,udini unaingia?
Njaa yaua wajomba,hata makombo watwaa?
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Mahakama sasa jumba, siasa kuzikamia,
Polisi na jambajamba, chama kukisaidia,
Tunaitafuta kamba,kunyonga demokrasia,
Budi kuzaliwa upya, wewe wajivua gamba?

Monday, September 19, 2011

Madebe yanayovuja

Jaza maji litajaa, pipalo linalovuja,
Ila muda huchukua, ni pande mbili za mrija,
Vigumu maji kukaa, kwani lazima kuvuja
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Gumba katu hatazaa, hata umvalishe koja,
Mbilikimo hatokua, hiyo siyo yake siraja,
Mbinafsi si mjamaa, ukubwa kwake kufuja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Kubaleghe majaliwa, haliji kwa kila mmoja,
Watu wengi wanakua, kwa mwili si kwa hoja,
Utotoni wanabakia, hata wapande daraja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Kuvunja ungo hatua, si mwanamwali kwa wanja,
Kuropoka si kujua, heri ya mvuta ganja,
Na ajira kuikwaa, bado kwa watu si hoja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Watu wataka majaa, viongozi wenye chaja,
Matatizo kuwavua, wakaiona faraja,
Na fursa kuwapatia, wakazipanda daraja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Uongozi ni tabia, na uzuri sio hoja,
Kichwa kikitangulia, kilichokosa faraja,
Mafuu huwateua, wakaleta masihara,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Wangapi wamesikia, ya Juja na maajuja,
Kuongoza makataa, dunia kuwa kioja,
Ndipo itakapoamuliwa, dunia kuwa mteja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Na debe huja kujaa, kisha huja kuvuja,
Raia watagharamia, viranjai wanaofuja,
Ni bara kwa Tanzania, hadi pia na Unguja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Viongozi tutapewa, wanaohitaji chaja,
Kama vile tumeishiwa, jamani fungeni mkaja,
Ni sinema ya sanaa, iko njiani inakuja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Hata nyanya zitapewa, ukubwa wenye vioja,
Wamiliki wa mkoa, wataonekana wakuja,
Na yatakayotokea, mkoa budi kuvuja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Nuru ikijaingia, wakazi sio waseja,
Haya watayakataa, na yote watayachuja,
Watapigania mkoa, uhuru wa kujikongoja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Ni kwa vipi Zanzibaa, leo eti twaitaja,
Ni nchi iliyokuwa, na rais kwao huja,
Na huku bara mkoa, viongozi ni wakuja?
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Ijiandae mikoa, miaka inayokuja,
Mkuu kumchagua, na sio wa kutajwa,
Kuwajibika ikawa, hiyo ndiyo yake hija,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Naililia Tanzania, nchi yangu ya wakuja,
Kasahaulika mzawa, ni nani wa kumtaja?
Na vyeo wanaopewa, wakutugeuza mateja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Naililia Tanzania, nchi yangu ya viroja,
Juu, chini atakua, chini kupewa daraja,
Na ukoloni mpya, kwa utandawazi waja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Awali takabalia, kwingine tusende hija,
Amerika kutokua, njia yetu ya hijara,
Na Ulaya sio Maka, wala Madina siraja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Karima kwako twalia, tupe imara viranja,
Uchungu wanaojua, wa kubeba wetu mkaja,
Hapa watakaotutoa, twende kuliko faraja,
Madebe yanayovuja, jaza maji yatajaa.

Saturday, September 10, 2011

Wakubwa wenye njaa

Wakubwa wenye njaa, kuua kwao si kazi,
Watu kwao ni dagaa,roho zetu wachuuzi,
Hawamwogopi Hafiizi,kiama wakikataa,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Mutafifini machizi, mafuu na makataa,
Kichwani wanazo ndizi,sio akili nakataa,
Mioyo yao viazi,rojo iliyorojea,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Usafiri kama kazi,unahitaji sheria,
Hata nao uchukuzi,viwango vinatakiwa,
Ila watu wapuuzi,nazi tumekwishakuwa,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Viongozi wabarizi,na ndege wajipandia,
Wakulima na wakwezi,shaurienu mtajua,
Hatuiachii enzi,chini kufuatilia,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Bandarini ni ajizi,rushwa inavyotembea,
Mtu akipewa andazi,chomboni hatoingilia,
Wakubwa na usingizi,mauti mwatuombea,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Kwenye meli viokozi,nadra kufumania,
Hapana na vizuizi,Mola atuhurumia,
Hapana usimamizi,udhibiti ni hadaa,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Wauaji si wanafunzi,walimu waliotimia,
Wabia wao viongozi,wote wanajichumia,
Na yao hayo machozi,ni mamba wanaolia,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Wenye njaa viongozi,balaa limetushukia,
Dhaifu wafanyakazi, shilingi wanaopewa,
Huliachia jahazi,Muumba kuangalia,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Hapanao wawekezi,malenga naulizia,
Meli zishehenezi,wingi kuja kupungua,
Abiria wabarizi,roho kutowakimbia,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Au ubia mwagenzi, kwa nguvu kuzitumia,
Wakaiza wawekezi, manowari kutuletea?
Au sheria bazazi, watu wanazikimbiya?
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Wenzetu wape makazi,ya Manani ya Alaa,
Viongozi kwa kitanzi,cha isiyokwisha njaa,
Wala usiwape uzi,hawana la kujitetea,
Kuua kwao si kazi, wakubwa wenye njaa!

Ana deni la maisha

Anayeliiba wazo, wivi hajajiepusha,
Kila wazo lina mwanzo, na aliyeliumbisha,
Watu walio uozo, hili lawastaabisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Ama lao tangulizo, Mola linamkanusha,
Fikra wazibebazo, wakubwa kufurahisha,
Muumba yuko likizo, ha\wezi wababaisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Kama dubu wa igizo, tabia inatapisha,
Hanao huo uwezo, jipya kuvurumusha,
Kazi yao ya chombezo, ya wengine kufatisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Hupenda mazungumzo, pia kuzisoma insha,
Wapate yako mawazo, ndo waweze kuanzisha,
Makala uzitoazo, kusoma huhakikisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Hujiona mzomzo, wanapoyabahatisha,
Wakafanza micharazo,na ubingwa kujitwisha,
Madokta wa msazo,hugeuka wakapasha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Hili kwangu si tatizo, hayo ni yao maisha,
Kilicho kwangu kikwazo, nasaba waziepusha,
Wamjue mwenye wazo, kumnukuu wabisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Hawahofu patilizo, Muumba kumkasirisha,
Hilo si lake agizo,hayo anayakanusha,
Haki lake angalizo,katika yetu maisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Ah, Bwana mwenye uwezo, bwana mwenye kulipisha,
Kuwa langu egemezo, kwa adili kunikosha,
Nisepe maangamizo, dunia hii ikiisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Wenye mali na uwezo, wajapo kujikausha,
Kunitenda kwa mabezo, yangu yakiwatajirisha,
Nipe ya kwako chelezo,nazidi kuniimarisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Waangaze wenye nazo, siha kuwatatanisha,
Na ajali mzomzo, zije kuwakaribisha,
Na siasa za uozo,wananchi kuja wachusha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Na wasio na mawazo, wizarani kuwashusha,
Kizazi kiwe tatizo,yawasumbue maisha,
Dhahabu iwe uozo,na fedha kuwatapisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Waliokupua wazo, fadhila wakarudisha,
Wamiminie radhizo, katika yao maisha,
Watunukie na tunzo, uzidi kuwaimarisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.

Ahadi wewe tulizo, katika haya maisha,
Nirahisishie himizo, maagizo kufatisha,
Niokoe na mizozo, peponi kunijulisha,
Anayelipora wazo, ana deni la maisha.