Friday, December 30, 2011

Uoga wenye faida

Uoga nitajitia, na magoti kutitia,
Kila ninapotambua, jambo nimeshakosea,
Udhaifu kuelewa, yakini umechangia,
Uoga wenye faida, kumuogopa Muumba.

Kwangu sikukusudia, shida kunisaidia,
Jambo likishatokea, lazima kulijutia,
Utakwa sijafikia, upungufu umejaa,
Uoga wenye faida, kumuogopa Muumba.

Na toba kuitubia, huruma kuhurumiwa,
Niombe kusamehewa, Muumba kunisikia,
Sio ya kwangu dunia, nini ninachotambia?
Uoga wenye faida, kumuogopa Muumba.

Njiani najipitia, mwisho wangu naujua,
Huko ninakoelekea, ndipo ninazingatia,
Msafara sijajua, kama nyuma wafatia,
Uoga wenye faida, kumuogopa Muumba.

Mwenyewe nilizaliwa, na pekee nitatua,
Watakaonipokea, uwanjani sijajua,
Naweza pekee ingia, njia nikaulizia?
Uoga wenye faida, kumuogopa Muumba.


© 2011 Sammy Makilla

No comments: