Wednesday, December 28, 2011

Pasipo televisheni

Redio isipokua, vigumu kuendelea,
Hapatazungumziwa, matatizo yalokua,
Na jinsi ya kutatua, mkoa kuendelea,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Wapi watazungumzia, muhimu yaliyokua,
Hoja wakazisikia, na aula kuchagua,
Kisha kujajipangia, na bajeti kuandaa,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Mikakati kuamua, mkoa unaofaa,
Mbinu wakazichambua, kazi rahisi ikawa,
Miaka ikapungua, afueni kutokea,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Gazeti lisipokua, wajinga wanachanua,
Hoja hawatazijua, ndiyo wataitikia,
Viongozi huchagua, wale wasiowafaa,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Wananchi wataibiwa, kila chao kilokua,
Rasilimali hupaa, na mali asili pia,
Na fedha hukwapuliwa, mchana wajionea,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Tovuti isipokuwa, ni mji uliovia,
Watalii hukimbia, hapo tena hawatakaa,
Kwingine huelekea, mawasiliano yakawa,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Televisheni kupwaya, mji huja kudumaa,
Katu hautaendelea, utazidi kusinyaa,
Na vijana husanzua, jijini kukimbilia,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Simu zisipoenea, mawasiliano huvia,
Vijana hupakimbia, kwingine wakaingia,
Kamwe hawatasalia, hata ukiwafungia,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Wakati tumefikia, maamuzi kuamua,
Redio za umma kua, kila mji Tanzania,
Ya mji kuzungumzia, na yanayotarajiwa,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Magazeti nayo pia, kila mji yatakiwa,
Habari zao kujua, mambo kuchangamkia,
Ya wengine kusikia, kurasa zinazofatia,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Tovuti tunatakiwa, kila kona kuchanua,
Ukienda kutembea, Google wajipatia,
Migawaha maridhawa, huduma ikazitoa,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Televisheni mbia, picha inatupatia,
Ni mengi tunayojua, papo hapo kujionea,
Ziara kujifanzia, hali chumbani twakaa,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Wakale hawakujua, umuhimu ulokua,
Uongo walichelea, gizani tukabakia,
Alamu katujalia, sasa zaangazia,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Ila kinachotokea, uchafu zinachukua,
Bado hatujajitambua, wenyewe twajiumbua,
Viongozi watakiwa, hili kuliangalia,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Zingekuwa za mkoa, vyemja zingedhibitiwa,
Kumoja kutolemea, na kwingine kuonea,
Na wanaosimamia, umiliki kuchukua,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!

Muhimu yangelikuwa, yanayozungumziwa,
Miji ije kuchanua, kama Ulaya ikawa,
Ikang'ara Tanzania, hadi huko Malaysia,
Pasipo televisheni, wazainiwa hujaa!


© 2011 Sammy Makilla

No comments: