Monday, December 26, 2011

Uongozi sio wizi ?

Uongozi nahofia, wivi waweza ukawa,
Kama wanaojipatia, wakubwa waliokuwa,
Wanyonge kudhulumiwa, na kidogo kuchukuliwa,
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Kiongozi akipewa, milioni kwa mamia,
Na hawa nao raia, kumi hawajaijua,
Huu sio wizi hua, mchna waendelea?
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Kumi na nane saa, daktari atumia,
Wagonjwa kuhudumia, bila hata kupumua,
Twashindwa kuwaangalia, wenyewe twajiangalia?
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Nesi kote huingia, haishi kujichafua,
Matapishi hufadia, na vinyesi kuchukua,
Bungeni unayekaa, chote hicho wachukua?
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Mwalimu choki yaja, machoni na kwenye pua,
Elimu anaitoa, kesho watakaomnyonyoa,
Hili twaliangalia, tunashindwa kuamua,
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Sahani mbili mwatwaa, tonge hatujalijua,
Na kisha mwagugumia, hakiwatoshi mwaonewa,
Ibilisi mmekua, binadamu twadhania?
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Kipimo mnachotumia, mimi bado kukijua,
Kiasi gani mwatwaa, na kiasi gani mwatoa?
Nini mnakichukua, na nini mwatupatia?
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Au mwavuna mamia, hata msikopandia,
Kwingine mwakupua, vya wengine vilokua,
Hakika nawashangaa, watu msiojijua,
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Kwa haya mtachukia, ukweli nawaambia,
Mungu mkimtambua, mtageuka tabia,
Nafsi kuzizuia, wengine kuwatangulia,
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Tazameni Malaysia, zamani walipoamua,
Viongozi kukataa, malipo yaliyozidia,
Wananchi kwanza kupewa, mtaji wakaendelea,
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Kisha wao kufatia, nchi imeshanyanyuliwa,
Nyie mwanza kutwaa, nchi inadidimia,
Na Mola kawaumbua, mafuriko kutokea,
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Sasa tunawashangaa, mwashindwa wajengea,
Hivi mnategemea, muujiza kutokea,
Fisadi walizochukua, kwanini kutotumiwa,
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

Nyumba ninawaambia, kwa fakiri ndio dawa,
Hili ukishampatia, mengine atajijua,
Ila mkiliachia, dhulumati tatajua,
Uongozi sio wizi, kama wananchi wanakosa?

No comments: