Friday, December 16, 2011

Nje tunajitangaza

Akilini haijakaa, utalii kutokua,
Kila nikifikiria, papo tulipokosea,
Laiti ningelijua, mimi ningegharamia,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Bandari na kupokea, bora kama zingekua,
Na viwanja vya kung'aa, kama Dubai vikawa,
Mamia wangelitua, na ajira kunyanyua,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Mandhari na maua, nchini zingetulia,
Ikawa ni lewalewa, kwa kila anayekaa,
Kwalo wangetusifia, wengine wakaingia,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Nchi ikiwa kinyaa, mtalii hatotua,
Na kama akijatua, haji tena kurejea,
Mbali ataishilia, na wengine kuwang'oa,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?


Nchi ikijisifia, maskini imekua,
Watu huinyanyapaa, kwingine kukimbilia,
Unanuka nakwambia, ufukara ni balaa,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Lazima kuuondoa, ufakiri Tanzania,
Heshima kujipatia, wengine kutotukataa,
Ndipo tutatembelewa, wenda na yote dunia,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Maji kuyagharamia, mahotelini kujaa,
Mabwawa kuogelea, bure yasijekukaa,
Starehe ni murua, watalii kwao dawa,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Uchafu kutofungulia, choo njiani kikawa,
Na wasiozingatia, si viongozi wa kufaa,
Kazi mbali futilia,na wengine kuchagua,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?


Barabara bora kua, salama kujisikia,
Watalii kushangaa, kila wanapotembela,
Njiani wasipojikwaa, na kukutwa na balaa,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Pikipiki zahofiwa, njiani zilizojaa,
Humo zinamopitia, daladala kufwatia,
Watu wanamopitia, pasi kushughulikiwa,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Njiani zafa sheria, kwao wanaotembea,
Zinalindwa motokaa, rushwa zinazochangia,
Watalii huambaa, nchi hivyo ikishakua,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Bei kuziangalia, ovyo tunazopangia,
Wengi huwashtua, kwingineko kuhamia,
Itakuwa ni ruia, milioni kufikia,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Uchumi kuunyanyua, vibaka wakapungua,
Zamani kuirudia, Zanzibar ilivyokua,
Vitu walirudishiwa, kila vilipopotea,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

Jamii ikichangia, na mapato kupatia,
Nao wakajisikia, ubia wameingia,
Utalii utakua, na nchi kuendelea,
Nje tunajitangaza, ndani tumefanya nini?

No comments: