Friday, December 16, 2011

Wabebwao na wakubwa

Mbeleko walofungiwa, mgongoni wakakaa,
Budi kujishikilia, kifua kutoachia,
Matuta huja fikiwa, na mashimo kuvamiwa,
Wabebwao na wakubwa, huondoka na wakubwa!

Bahari kweli hujaa, na kupwa kunafatia,
Kutoka na kuingia, huwa hiyohiyo njia,
Na neema na balaa, ni hiyohiyo jamaa,
Wabebwao na wakubwa, huondoka na wakubwa!

Mbebwapo shikilia, na sio kuning'inia,
Ukila unavyopewa, vichungu hutochukia,
Na juu ukishapaa, si vibaya kutambaa,
Wabebwao na wakubwa, huondoka na wakubwa!

Ukibebwa zingatia, kushushwa itafikia,
Salama utagundua, taratibu kujiachia,
Na kujenga mazoea,hali kutokukataa,
Wabebwao na wakubwa, huondoka na wakubwa!

No comments: