Wednesday, December 28, 2011

Kiswahili mama yetu

Uchina na Malaysia, mamao wanamlea,
Tena wanajivunia, wazidi kuendelea,
Hatua waliyofikia, mama kawasaidia,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Majuha tuliokua, ung'eng;e twang'ang;ania,
Twadhania ni dunia, Kiingereza kujua,
Nchi zinadidimia, tutakujajionea,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Jioni imeshakua, magharibi yaingia,
Mashariki laanza jua, ndio kwanza latokea,
Na kwa wanalojijua, hili wataling'amua,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Mashariki kunafaa, kwenda kujinyanyua,
Magharibi kutembea, wataali kuja kuwa,
Vichache kuokotea, vya kuja kujazilia,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Hivyo tungelianzia, nyumbani kutia paa,
Kiswahili jua kua, havi vyuo kutumia,
Na kisha kufyonzea, maarifa yakakua,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Uchina ninawaambia, elimu zote watia,
Kwenye lugha watumia, kwa kazi na kufundishia,
Hakuna wasilojua, na wengi hawajawajua,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Malaysia nao pia, lugha wameipania,
Kote wanaitumia, toka huko chekechea,
Nini utachowambia, ksiwe kimalaysia?
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Sisi mama twamchezea, kwa rushwa kuzipokea,
Lugha kutoitumia, Kiingereza kubakia,
Hali wote tunajua, wazito kushikilia,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Ilivyo sasa dunia, lugha zao watumia,
Kisha wanazifungua, maabda zikajaa,
Lugha kufundishia, mbalimbali zilokua,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Lugha wana huchagua, ipi ya kuichukua,
Mbili tatu zinakua, zote vyema akajua,
Maabara hutumia, miezi michache waa,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Kizamani twabakia, miaka kuitumia,
Wenzetu fumba fumbua, lugha mpya hujua,
Maabara kutumia, shuleni zinazokaa,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Mkakati hutumia, dunia kuangazia,
Wapi kunakofaa, bidhaa kuzichukua,
Na elimu kuitwaa, enzi inazozifaa,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Ila budi kujaliwa, viongozi wakufaa,
Baraka wanaochukua, na uchaMungu kupewa,
Majina watakapewa, nyuma yawezayo bakia,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Na sio wapita njia, waigizao sanaa,
Wamekuja kutumia, na matumbo kuchumia,
Na sio kutumikia, watu wakawanyanyua,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Bishara ukizijua, Mola hukufunulia,
Za kuzipitia njia, watu uje kuwafaa,
Na lugha yao kukua, ikaikubali dunia,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!

Aidhawanaotubia, naye kumgeukia,
Rehema zimemjaa, na huruma kajaliwa,
Wadogo huwasikia, kama wakubwa wakiwa,
Kiswahili wetu mama, wana tumemkimbia!



© 2011 Sammy Makilla

No comments: