ZIMEFIKA zama hizi, hadhi wawe nayo wezi,
Na wakubwa majambazi, inshallah viongozi,
Walinzi wawe mijizi, wenye sheria hifadhi,
Mamlaka kama jizi, ya wezi kaziye wizi !
Na wa dini viongozi, kugeuka walanguzi,
Dini ziwe uchuuzi, bidhaa na matanuzi,
Busara iwe masinzi, na hekima kuwa nazi,
Mamlaka kama jizi, ya wezi kaziye wizi !
Malaya wawe wajuzi, wa kazi sio mapenzi,
Vyeo viwe fumanizi, wanone kimaangamizi,
Watajileta mabuzi, kuchinjwa kwenye makazi,
Mamlaka kama jizi, ya wezi kaziye wizi !
Ujaji huwa ni vazi, si utenzi bali hadhi,
Haki wawe wachuuzi, na wa chini dumuzi,
Yakaenea maradhi, pasiwe nayo hifadhi,
Mamlaka kama jizi, ya wezi kaziye wizi !
Wajinga wapewe kazi, na pengine uongozi,
Kazini kupanda ngazi, iwe kama utelezi,
Ufanisi jinamizi, kuzama isiwe kazi,
Mamlaka kma jizi, ya wezi kaziye wizi !
Waandishi na watunzi, wawe kwao waigizi,
Uongo waudarizi, liwe lao kuu vazi,
Keki likawa andazi, fumanizi, ugunduzi,
Mamlaka kama jizi, ya wezi kaziye wizi !
Urongo uwe ujuzi, wautaka viongozi,
Na umma kuwa zoezi, hadaa kuzimaizi,
Nchi isiwe majazi, bali shari na ajizi,
Mamlaka kama jizi, ya wezi kaziye wizi !
Kipendwacho kukabidhi, nusu yake maamuzi,
Ikafanza matanuzi, pato lenye ubaguzi,
Walewe utandawazi, na wa nje majambazi,
Mamlaka kma jizi, ya wezi kaziye wizi !
Huchaguliwa viazi, vikapika maandazi,
Na wasioenda kozi, wakawa ni wakufunzi,
Viatu kuwa kubadhi, wakavaa wanawenzi,
Mamlaka kama jizi, ya wezi kaziye wizi !
Wenye hoja kuwa mbuzi, waheshimiwa kwa ngozi,
Yakakwama mageuzi, uchama kushika uzi,
Tozo hili hatutozi, wajao watamaizi,
Mamlaka kama jizi, ya wezi kaziye wizi !
© 2011 Sammy Makilla
Wednesday, December 28, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment