Wednesday, December 28, 2011

Mwafrika si fukara

Kila ukimchunguza, Mwafrika anaweza,
Kuna kinachomlemaza, maisha yakamkwaza,
Hakuna anayewaza, jambo hilo kutengeza,
Mwafrika si fukara, msaada yatulemaza!

Ukoloni wa kuzoza, watu walishamaliza,
Na tunachokibakiza, wakoloni waongoza,
Si watu wa kutengeza, bali juu kujikweza,
Mwafrika si fukara, msaada yatulemaza!

Kuzalisha si waweza, ila kula na kusaza,
Ni watu wa kumaliza, wala sio wa kuanza,
Kazi ni kubangaiza, wala si nchi kugeuza,
Mwafrika si fukara, msaada yatulemaza!

Sio watu wa kujaza, ila daima kupunguza,
Ni watu wa kupuuza, fanyeni mnayoweza,
Mzawa kimbia giza, mwenyewe kujiendeleza,
Mwafrika si fukara, msaada yatulemaza!

Miaka mtamaliza, mbele hamtajisogeza,
Viongozi wana funza, hawawezi kuongoza,
Ukubwa kwao ni chaza, kuvuna wasichotunza,
Mwafrika si fukara, msaada yatulemaza!

Someni mnaoangaza, na wengine kuwafunza,
Labda ije miujiza, Mzungbu keshawalemaza,
Neema itawaiza, kwa rushwa kuwapumbaza,
Mwafrika si fukara, msaada yatulemaza!

Sifa wanaojijaza, kusonga hawataweza,
Watu wa kufululiza, wenyewe wakajikuza,
Hutuacha tulipoanza,kama si kutudumaza,
Mwafrika si fukara, msaada yatulemaza!

Cha mzawa wanabeza, na Mzungu kumkuza,
Uchina inawabeza, na wengine kuwaiza,
Majuha wa kupumbaza, wengine wanawajuza,
Mwafrika si fukara, msaada yatulemaza!

Azizi unayeweza, tupe wasiolemazwa,
Nchi kuiendeleza, ugumu ukakatiza,
Ya heri kufululiza, hadi juu kutukweza,
Mwafrika si fukara, msaada yatulemaza!


© 2011 Sammy Makilla

No comments: