Hivi leo ni balaa, viongozi tunajua,
Ila kazi kuwatoa, kwa wanavyong'ang'ania,
Na sheria watumia, halali zisizokua,
Mamlaka ya wananchi, katiba izingatie!
Ujibari wajitia, mno tumewaachia,
Mimi kweli nashangaa, tajiri na muajiriwa,
Ang'aka muajiriwa, tajiri kumtimua,
Mamlaka ya wananchi, katiba izingatie!
Kinyume ingelikuwa, kufukuzwa mwajiriwa,
Kazi akiitibua, wengine wakachukua,
Afrika yazubaa, wazidi kutuonea,
Mamlaka ya wananchi, katiba izingatie!
Wananchi hawajajua, nguvu waliyojaliwa,
Wabaya wavumilia, na wezi waliokua,
Dhima wanaotumia, kwa ya kwao manufaa,
Mamlaka ya wananchi, katiba izingatie!
Katiba kuifumua, vipengele vikajaa,
Hili kusimulia, jinsi ya kuwaongoa,
Viongozi wasiofaa, hata wakichaguliwa,
Mamlaka ya wananchi, katiba izingatie!
Amgaza wamasheria, katiba kujatufaa,
Sio tena kuchezewa, na kazi wasiojua,
Muda kutupotezea, hatukuja kutembea,
Mamlaka ya wananchi, katiba izingatie!
Mamlaka kuchukua, madaraka kuachia,
Na mifumo ya kufaa, viongozi kukataa,
Huu wakati radhia, tusije kuuachia,
Mamlaka ya wananchi, katiba izingatie!
Bwana twakusujudia, Maliki uliyekua,
Uiongozayo dunia, iongoze Tanzania,
Viongozi kutufaa, watakaotunyanyua,
Mamlaka ya wananchi, katiba izingatie!
© 2011 Sammy Makilla
Friday, December 16, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment