Paka wa mheshimiwa, naye ni mheshimiwa,
Awe shume tena duni, angali mheshimiwa,
Atatamba mitaani, kwa wenzaake hayawani,
Paka wa mheshimiwa, naye ni mheshimiwa!
Utu kitu cha hisani, mwerevu atabaini,
Utukufu hathamini, ajiongeze thamani,
Hujishusha sana chini, akawa ni mtu duni,
Paka wa mheshimiwa, naye ni mheshimiwa!
Ila kama afkani, hujikweza ardhini,
Juu anaposakini, mwishowe hufichwa ndani,
Tambo na zake razini, ziwe hazina auni,
Paka wa mheshimiwa, naye ni mheshimiwa!
Nafsi kuwazaini, pepo iko duniani,
Nyota wakaziamini, na kuwapa tumaini,
Ila siku ikighani, hujikuta majinuni,
Paka wa mheshimiwa, naye ni mheshimiwa!
Ni mapaka machakani, yasiyo nayo imani,
Wenyewe hujizaini, kwa yaliyo akilini,
Wasojua kwa yakini, vyote huishia chini,
Paka wa mheshimiwa, naye ni mheshimiwa!
Paka wake sultani, hujiongezea shani,
Utukufu kubaini, na ubora kuamini,
Akajiona peponi, wakati yu duniani,
Paka wa mheshimiwa, naye ni mheshimiwa!
Haya sikusimuliwa, ila nimejionea,
Na kila nikichunguwa, nazidi kulielewa,
Ila wanaopitiwa, sio wanaojijua,
Paka wa mheshimiwa, naye ni mheshimiwa!
© 2011 Sammy Makilla
Sunday, January 1, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment