Sunday, January 29, 2012

Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Bahati wasiopewa, hupata kikapotea,
Yalo mema huitiwa, nao wakayakimbia,
Pepo hutengenezewa, moto wakauchagua,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Asali huiambaa, shubiri wakachagua,
Neema huikemea, balaa wakaridhia,
Nusura huikimbia, maasi wakaingia,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Chumvi huichagua, sukari ikitakiwa,
Maji huyazidishia, ukavu unapotakiwa,
Gia ya nyuma hutia, ya mbele ikitakiwa,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Chini hujifukia, juu wanapotakiwa,
Gizani hukomelea, nuru nje imejaa,
Milioni hutumia, wakati yatosha mia,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Uoni huwapungua, uongo ukiwavaa,
Ya kweli huyakataa, uzaini kuridhia,
Juto mjukuu huwa, Joti wakamuachia,
Huchota maji bahari, wakacha maji baridi !

Januari 29, 2012
Dar es Salaam

No comments: