Thursday, January 12, 2012

Mwafrika taahira,

Napaswa haya kujua, wanangu kuwaambia,
Nini kilichotokea, hadi fakiri tukawa,
Haya tumejitakia, au sisi twaonewa?
Mwafrika taahira, kuendelea hawezi ?

Nini kilichopungua, hapa kwetu Tanzania,
Ardhi tumejaliwa, rutuba iliyojaa,
Na madini yametiwa, ndani yanaelemea,
Mwafrika taahira, kuendelea hawezi ?

Mito kote hutambaa, na maziwa yamejaa,
Visima twajichimbia, na chemchemi hukua,
Lakini twalia njaa, kila tukiamkia,
Mwafrika taahira, kuendelea hawezi ?

Akili hatukupewa, makapi tunatumia?
Au tumehujumiwa, zezeta tumeshakua?
Wengine watutumia, na hatwezi jihudumia,
Mwafrika taahira, kuendelea hawezi ?

Shuleni tukipitia, sifa tunazichukua,
Kazini tukiingia, utoto tunarudia,
Hatuna la kuvumbua, wala jipya kuzua,
Mwafrika taahira, kuendelea hawezi ?

Kinyaa tumeshakua, hata kwa tuliowazaa,
Hawaeshi kuulizia, nini kinachoendelea?
Kimya chawasumbua, maiti watudhania,
Mwafrika taahira, kuendelea hawezi ?

Sifa twajipalilia, vya ushuzi vilokua,
Na vichwa kutanua, hata kwa tusiojua,
Kisirani tumekua, ukubwa watuzuzua,
Mwafrika taahira, kuendelea hawezi ?

Ulaya tukiingia, vipofu tunabakia,
Hatuoni cha kufaa, nchi kuja iinua,
Twabaki twashangaa, majuha tunabakia,
Mwafrika taahira, kuendelea hawezi ?

Ndio kisa kuulizia, tutafute kujijua,
Kwani tusipojijua, katu hatutaendelea,
Fakiri tutabakia, watumwa wa majaliwa,
Mwafrika taahira, kuendelea hawezi ?

No comments: