Friday, January 13, 2012

Ni nani wa kumwogopa

Nitamwogopa mtu gani, kama Mola yuko nami,
Nani ni mwenye mizani, awezaye kunihami,
Nani ni mwenye hisani, asiye nao umimi?
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

Huyu siye tu Manani, bali ni wa kwangu Ami,
Nikiwepo duniani, wa kwanza kwenye ulimi,
Naomba yake auni, kuchunga wangu usemi,
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

Na kama nikiwa mgeni, Uturuki na Ajemi,
Naomba yake ihsani, aniepushe na watemi,
Nuru iwepo mbeleni, na nyuma ikinihami,
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

Nuru iwepo usoni, kuiepuka jahimi,
Kadhalika na machoni, uoni uwe wa lami,
Naye bila kusaini, iwe kitu sikifumi,
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

Nikuze yangu imani, katika hii jamii,
Upole na umakini, ujaze wangu ulimi,
Katika feli na kani, pasiwe kitu sipimi,
Ni nani wa kumwogopa, kama Mola niko naye?

No comments: