Unayaona umati, mengi yasiyo ya dhati,
Na kwazo mita na futi, vipimo wanadhibiti,
Waipate ithibati, isiyo na usaliti,
Ndio huu uamsho,
ya kwetu ni tofauti:
Na nguo yetu ya mwisho,
ni sanda na sio suti !
Wanaokimbia shoti, kwa nafsi na baiti,
Wakauata umati, wazidi kushuka chati,
Awaona Muqliti, na kwake hawa hayati,
Ndio huu uamsho,
ya kwetu ni tofauti:
Na nguo yetu ya mwisho,
ni sanda na sio suti !
Sijui mwisho ubeti, na nukta siiwati,
Njia sio katikati, hayo yanakosa dhati,
Picha watu hawapati, na bishara haileti,
Ndio huu uamsho,
ya kwetu ni tofauti:
Na nguo yetu ya mwisho,
ni sanda na sio suti !
Maisha ni mkakati, na kufanza utafiti,
Ngome si ya moja geti, njia nyingi ni shuruti,
Na akili mahluti, haziachi kudhibiti,
Ndio huu uamsho,
ya kwetu ni tofauti:
Na nguo yetu ya mwisho,
ni sanda na sio suti !
Lawama hazifukuti, wala kuling'oa bati,
Ustawi si bahati, ni kunuia kwa dhati,
Mabadiliko huleti, bila ya kujizatiti,
Ndio huu uamsho,
ya kwetu ni tofauti:
Na nguo yetu ya mwisho,
ni sanda na sio suti !
Kamati kubwa kabati, au sefu na dawati,
Utakayo huyapati, hupata yaso garanti,
Fikra sio mashuti, ni nyavu kama si neti,
Ndio huu uamsho,
ya kwetu ni tofauti:
Na nguo yetu ya mwisho,
ni sanda na sio suti !
Waogao hawatoti, ila kwa wenye makoti,
Vipande hivi si doti, na miaka haitokoti,
Wakati hatuukuti, hata kwa ndege na jeti,
Ndio huu uamsho,
ya kwetu ni tofauti:
Na nguo yetu ya mwisho,
ni sanda na sio suti !
Kiwasheni kibiriti, nuru iwake katiti,
Na moto ukidhibiti, mwanga usitusaliti,
Maisha si kismati, ila ni kujizatiti,
Ndio huu uamsho,
ya kwetu ni tofauti:
Na nguo yetu ya mwisho,
ni sanda na sio suti !
Sunday, January 8, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment