Wacha wale raha leo, kesho watalia sana,
Maisha kama mgao, na watu hupokezana,
Ni wachache wajuao, neema zisizosana,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !
Hadithi na mapokeo, haya yameona sana,
Na dunia kama chuo, weledi si wengi sana,
Na mambo yawapitayo, huja mwishoni kuona,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !
Wa Pwani kwenye mwambao, bahari husema sana,
Kungwi na wawaleao, kwao yanajulikana,
Na vyungu wainjikao, sio hao wabebao,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !
Mambo yataka tambuo, utotoni na ujana,
Wazazi waelewao, haya huwafunza wana,
Wasio wakati nao, hubaki wakapishana,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !
Na watenzi wajuao, tungo zao za maana,
Husema maneno hayo, na kuandika kwa kina,
Ila ni wajaliwao, huweza kuja yaona,
Wacha wale raha ndogo, kesho watakonda sana !
Saturday, January 14, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment