Friday, January 13, 2012

Pambazuka Afrika

Pambazuka Afrika, kwaanza kuendelea,
Wazungu kwao watimka, ajira kukimbilia,
Nchi zaweza jengeka, akili tukitumia,
Pambazuka Afrika, sasa ni mbele kwa mbele!

Viongozi Afrika, watakiwa kulijua,
Waache kubabaika, maamuzi kuamua,
Kwenda hadi Amerika, vibarua kuchukua,
Pambazuka Afrika, sasa ni mbele kwa mbele!

Ulaya wanateseka, kwa ajira sio njaa,
Watu wanaweweseka, akili kutozitumia,
Na kubwa wanalolitaka, wapate kuajiriwa,
Pambazuka Afrika, sasa ni mbele kwa mbele!

Rasilimali twataka, za watu zilizokua,
Mali asili hakika, haya tulishajaliwa,
Hivi vikiunganika, Afrika itapaa,
Pambazuka Afrika, sasa ni mbele kwa mbele!

Matatizo kuyasaka, watu yanayosumbua,
Kisha idara kuweka, elimu-kazi kuzaa,
Na iwe kuelimika, ni tatizo kutatua,
Pambazuka Afrika, sasa ni mbele kwa mbele!

Vijana wasoajirika, sasa watatamanika,
Kesho yetu kugeuka, ikawa ni ya hakika,
Majogoo wakawika, watokao Afrika,
Pambazuka Afrika, sasa ni mbele kwa mbele!

No comments: