Sunday, January 29, 2012

Uonevu ukizidi

BASHIRI macho hafungi, na huona kila jambo,
Msije kula mirungi, muone yasiyo tambo,
Ya mja hayamchengi, kwa sauti au wimbo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Kinyonga kwake haringi, ndiye aliyempa umbo,
Humbadili kwa rangi, adawa kukwepa mkumbo,
Na kwa mapozi ni kingi, ashinda hata mgambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Viumbe walio wengi, ni wadogo kwa maumbo,
Na si watu wa mitungi, wala kwa wingi mapambo,
Hutafuta la msingi, mengine kwao vijambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Lakini mlangilangi, yao yaendayo kombo,
Hutafuta kama nungwi, yaumizayo matumbo,
Kunao wavuta bangi, wajifanyao ni Rambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Nao wenye mali nyingi, huwatumia mgambo,
Hawana chao kichungi, haki kuwa mtarimbo,
Watakayo ni shilingi, wengine kula vikumbo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Tamaa hawajivungi, hukaa nawe kitambo,
Hutumia nguvu nyingi, kuzikuza zao tambo,
Hata wenye fungu jingi, huzama kwenye mkumbo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Omwami na kina mangi, wanayaguna mafumbo,
Kadhalika na wasangi, na watani zao Rombo,
Hukiondoa kigungi, hata wakenda Urambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !

Mwana muulize Dingi, kama naye ana jambo,
Nawe uwe ni mchungi, kunusuru lako tumbo,
Na ukaushe matangi, kwa dhuluma yake chambo,
Uonevu ukizidi, Mola huleta nusura !


Januari 29, 2012
Dar es Salaam

No comments: