LEO wanaozaliwa, hawajui kuongoa,
Kuongoza wafifia, na mikakati yavia,
Ujanja wanatumia, akili zimefubaa,
Wengine wamelaniwa, mabavu wanatumia,
Ndumilakuwili wawa, na wengine kwingilia,
Waidhulumu dunia, twazidi kuchanganyikiwa,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Wakubwa walojaliwa, haramu wametumia,
Halali kuibagua, na heri kuyoyomea,
Sasa kilichobakia, ni siasa za hadaa,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Walonacho wanatwaa, wasonacho kutumia,
Katika kumi wakiwa, wanane wadhulumiwa,
Mkoloni katwachia,ulaji wa kufukua,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Wachache walobaki, wazungukwa na hadaa,
Sifa wakilundukiwa, uongo watauchukua,
Ukweli wakakataa, nje unapotokea,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Vioo vimeshapotea, wapi kujiangalia ?
Maji wanayatumia, sura yanayochafua,
Huwa kinachotakiwa, sio kweli na usawa,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Madubu waingilia, vitisho kuvitumia,
Wengi wanaohofia, lisofaa huridhia,
Mkuku kuchukuliwa, watu yasiyowafaa,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Kaskazini ingawa, wapo tusiowajua,
Kimya wanasimamia, bila sifa kungojea,
Nchi zao zinakua, na amani imejaa,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Afrika kuna njaa, hata viongozi pia,
Ovyo wanavibugia, hata na vyao raia,
Kisha wanasingizia, hilo wanalosingizia,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Na laana zaingia, unafiki ulokua,
Safi wanayemjua, hutaka kumchafua,
Mdogo akitokea, chini humshindilia,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Ni uroho na tamaa, yaitawala dunia,
Ukubwa wakimbiliwa, bila kazi kuijua,
Mangimeza watumiwa, wananchi kuwaibia,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Matapeli wamejaa, viongozi waingiwa,
Wakija kushtukia, nchi wameiachia,
Kwa bei iliyokuwa, sawa na sifuri kuwa,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Matajiri wakamia, uongozi kuutwa,
Si kwa watu kuwafaa, ila wenyewe kupaa,
Na matanuzi kuvaa, kwa ukubwa kuuchukua,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Viongozi wa raia, hakuna alobakia,
Madiba kujiondoa, utupu tumeachiwa,
Uchi sasa tunahaha, hapana penye staha,
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Vijiji twavikimbia, uchungu ulikojaa,
Na madhila yamejaa, waweweseka raia,
Kama tungewanyanyua, nafuu ingelikua
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Na Mola twamtania, kwa uongo na hadaa,
Kachoka kuvumilia, na sisi si mashujaa,
Zitapozuka balaa, wapi tutakimbilia?
Yafilisika dunia, hakunao viongozi !
Tuesday, January 10, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment