AFYA ukijaliwa, hilo ni deni tambua,
Yafaa kuitumia, kwa yale yatayokufaa,
Siku zikishatimia, thawabu kujivunia,
Afya yako ni deni !
Naam utashangaa, haya ukiyasikia,
Bali nakuhakikishia, ni ukweli ulotimia,
Kama hukuyajua, macho nimekufungua,
Afya yako ni deni !
Ni deni ninakwambia, utakuja kudaiwa,
Muumba unayemjua, budi kuliulizia,
Nawe kumsimulia, jinsi ilivyokuwa,
Afya yako ni deni !
Askari hudaiwa, na wao pia raia,
Ole wao watumiwa, na hawatasaidiwa,
Kila wakisingizia, kidole kwa hurejea,
Afya yako ni deni !
Nguvu waliotumia, wanafunzi kuwavaa,
Au wapole raia, waliojikutania,
Na maandamano yakawa, salama yenye ulua,
Afya yako ni deni !
Husimulia jamaa, kisha kuhukumiwa,
Afya waliitumia, vibaya isivyofaa,
Motoni wataingia, huku wakijijutia,
Afya yako ni deni !
Nesi wanaowaua, wagonjwa huku wajua,
Nao watasimulia, huku ukiwa wakiwa,
Wasiamini kujua, wenye aya wayajua,
Afya yako ni deni !
Madaktari nao pia, kitabu kitasogea,
Ukweli kuugundua, sivyo walivyoamua,
Nafsi kutangulia, Muumba hakukusudia,
Afya yako ni deni !
Wanasiasa wakiwa, zamu itawafikiya,
Midomo itanyamaa, la kujibu kutojua,
Midomo itaamua, yenyewe kujisemea,
Afya yako ni deni !
Afya waliyopewa, wenyewe walitumia,
Kingi wakajimegea, chakula kilichokuwa,
Dhuluma wakaamua, vya watu kuvichukua,
Afya yako ni deni !
Saturday, January 7, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment