Monday, March 26, 2012

Ingekuwa uranium ?

Watu chini huanzia, sio juu hutokea,
Msingi usipokuwa, jengo halitobakia,
Tsunami ikiingia, hakuna cha kubakia,
Vinyesi barabarani, sasa twafungulia,
Zimesinzia sheria, hazichukui hatua,
Uranium ingekuwa, inavuja kwenye njia:
Nini kingelitokea ?

Kuzuri kulikokuwa, wa juu wankokaa,
Makwetu huku udhia, wa kawaida raia,
Uwekezaji wavia, heshima imepungua,
Vinyesi barabarani, sasa twafungulia,
Zimesinzia sheria, hazichukui hatua,
Uranium ingekuwa, inavuja kwenye njia:
Nini kingelitokea ?

Watalii twalilia, twakosa hata maua ?
Bustani zapotea, ya ikulu yabakia,
Muhimu kujishangaa, udhia tulivyokuwa,
Vinyesi barabarani, sasa twafungulia,
Zimesinzia sheria, hazichukui hatua,
Uranium ingekuwa, inavuja kwenye njia:
Nini kingelitokea ?

Watu viguu na njia, nini kitaangaliwa?
Muda wazidi potea, viraka tumebakia,
Mahandaki yamekuwa, njia katika mitaa,
Vinyesi barabarani, sasa twafungulia,
Zimesinzia sheria, hazichukui hatua,
Uranium ingekuwa, inavuja kwenye njia:
Nini kingelitokea ?

Mlo juu mwatakiwa, haya kuja jionea,
Kwa miguu kutembea, mpate wetu udhia,
Labda mtafikiria, makwenu mkirejea,
Vinyesi barabarani, sasa twafungulia,
Zimesinzia sheria, hazichukui hatua,
Uranium ingekuwa, inavuja kwenye njia:
Nini kingelitokea ?

Mabasi yetu balaa, TB yatutishia,
Abiria wanavyojaa, kwambukizana si nia,
Ila nchi yatuachia, wenyewe kuteketea,
Vinyesi barabarani, sasa twafungulia,
Zimesinzia sheria, hazichukui hatua,
Uranium ingekuwa, inavuja kwenye njia:
Nini kingelitokea ?

Muhimbili wasifiwa, mbu wamezawadiwa,
Ni wakubwa walokuwa, utandawazi waingia,
Kimataifa wadaiwa, hadhi waweza chukua,
Vinyesi barabarani, sasa twafungulia,
Zimesinzia sheria, hazichukui hatua,
Uranium ingekuwa, inavuja kwenye njia:
Nini kingelitokea ?

Vipofu tumeshakuwa, hatuuoni udhia,
Viziwi wa kusikia, ukweli twaukataa,
Husema tusiyojua, twaacha tunayojua,
Vinyesi barabarani, sasa twafungulia,
Zimesinzia sheria, hazichukui hatua,
Uranium ingekuwa, inavuja kwenye njia:
Nini kingelitokea ?

Bila ya kutengemaa, ya chini yalokuwa,
Usia nawaachia, wana mwaja kuwaua,
Na hukumu zatakiwa, toka sasa kwandaliwa,
Vinyesi barabarani, sasa twafungulia,
Zimesinzia sheria, hazichukui hatua,
Uranium ingekuwa, inavuja kwenye njia:
Nini kingelitokea ?

No comments: