NCHI ya kubarikiwa, wazee huangalia,
Wala haitawatumia, kwa zaini na sanaa,
Ila lazima ikiwa, nalo hilo walijua,
Tuwakumbuke wazee, sio wakati wa shida:
ila daima dawamu!
Nchi hii yaumia, wazee kutojaliwa,
Ni wana wanaachiwa, fukara kuangalia,
Watoto wasipokuwa, maisha kizaazaa,
Tuwakumbuke wazee, sio wakati wa shida:
ila daima dawamu!
Radhi inatukimbia, nafsi kutupalia,
Ya kwetu kuangalia, ya kwao yawe yaviaa,
Utu umetupotea, roho mabya zimekuwa,
Tuwakumbuke wazee, sio wakati wa shida:
ila daima dawamu!
Mateso yawaumbua, na dhiki zilivyojaa,
Kula kwao kubabia, na afya yao hatia,
Nani wa kuwaangalia, nchi ikishakataa?
Tuwakumbuke wazee, sio wakati wa shida:
ila daima dawamu!
Na aibu tusokuwa, twenda kuwakimbilia,
Ya kwetu kuwaambia, na yasiyowasaidia,
Mimi hili nashangaa, tena ninalikataa,
Tuwakumbuke wazee, sio wakati wa shida:
ila daima dawamu!
Uzee tungetambua, ndoo mizizi huanzia,
Imara wasipokuwa, nchi yote huungua,
Na kinachobakia, majivu tu yatakuwa,
Tuwakumbuke wazee, sio wakati wa shida:
ila daima dawamu!
Hili ninaling'amua, siachi wanyenyekea,
Masikini walokuwa, kila wanaponijia,
Kidogo nikakitoa, kwa hali kuwajulia,
Tuwakumbuke wazee, sio wakati wa shida:
ila daima dawamu!
Nchi ingelitambua, hazina iliyokuwa,
Vyema ikiwatumia, mbali twaweza fikia,
Kadri kuinyanyua, nchi yetu Tanzania,
Tuwakumbuke wazee, sio wakati wa shida:
ila daima dawamu!
Bashiri twamlilia, wazee kusaidia,
Nafuu kwao ikawa, huko tunakoendea,
Na nchi ikajaliwa, mamboye kutengenea
Tuwakumbuke wazee, sio wakati wa shida:
ila daima dawamu!
Sunday, March 11, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment