Tuesday, March 27, 2012

Kicheko usichocheka

Hukuumiza moyoni, kicheko usichocheka,
Kichomi kiwe mbavuni, kifua kikateseka,
Raha uwe huioni, uzidi kukasirika,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

Watu huwa mashakani, na shaka haijafika,
Sikuzote taabani, watakuja kudhurika,
Na wenye mali ndani, kuhofu wafilisika,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

Wenye uzuri mwilini, wagwaya watachujuka,
Uzuri wakathamini,kuliko kilichowaweka,
Wakaishiwa imani,kwa sumu wakapambika,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

Na wanaojiamini, akili zimepevuka,
Wakajiweka kundini, kwa akili kuhesabika,
Hawaishi tathmini, ya kama wanawehuka,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

Wazima huwa shakani, maradhi yatawashika,
Ikawa zao mizani, riziki zinapimika,
Na mengine abadani, hawataki kuyashika,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

Mtaji wanaoghani, miradi kukamilika,
Huyatafuta madeni, kichwani yakabebeka,
Hofu yao duniani, wasije kuanguka,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

Mimi nimebaki ndani, shauri ninaliweka,
Namuachia Manani, hali yangu kutunzika,
Nangojea hisani, kulishwa na kunivika,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

Nami naishika dini, nisome na kupambika,
Nipate kuwa kundini, wasomi wasioridhika,
Katika yake Qurani, kuijua na hakika,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

Nataka ijenga dini, kwa ridhaa ya mhusika,
Ya Allah, biidhini, ninaiomba hakika,
Na Maashallah mwakani, nimalize robo njia,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

Nautafuta utani, utakaostahika,
Nimchekeshe Mughni, na wengine kadhalika,
Maisha yawe laini, tena pasi kusumbuka,
Kicheko usichocheka, hukuumiza moyoni!

No comments: