Thursday, June 28, 2012

Wahuni wakitawala



Inafaa kulijua, hali inapotokea,
Usalama 'kitumiwa, raia kugeukia,
Mbali hatutafikia, mabavu yatatuua,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Mnyama akiachiwa, damu akajilambia,
Utamu atanogewa, kila sikukurarua,
Nawe hukugeukia,  ndugu pia na jamaa,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Huua demokrasia, unazi ukauzua,
Ufashisti kuzua, na watu kuwabagua,
Siasa zikaingia, maendeleo kuvia,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Haki watazichumbua, na uhuni kuutia,
Vipigo vikaingia, na sumu watu kupewa,
Tindikali kutumiwa, usoni wakamwagiwa,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Uchu ulivyowajaa, rahisi sana kuua,
Ila kwa yao tamaa, waweze kujipatia,
Hayo wanayofikiria, uungu wakaujua,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Uwizi wataingia, vya watu wakachukua,
Na vilema kututia, hatia tusiokuwa,
Nami ninavyowajua, hapo hawataishia,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Njiani wataingia, kuziteka motokaa,
Porini wakakutia, kisha ukasulubiwa,
Huko wakakuachia, kufa au kujiokoa,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Makwenu wataingia, vioja kuwafanzia,
Ni wahuni kwa kuzawa, na pia kwa kutumiwa,
Mungu wamemkimbia, sanamu kujiumbia,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Iko njiani Syria, wahuni mkiachia,
Nchi wataibomoa, kwa kushoto na kulia,
Wakawasagwa raia, kama ng'ombe vile kuwa,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Silaha watatumia, raia wakawaua,
Na kisha kusingizia, magaidi wamekuwa,
Na juu wachekelea, wasiwasi kutokuwa,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Ni watu waliolaniwa, iblisi awajua,
Kamba amewaachia, wenyewe kujinyongea,
Lakini kujitambua, sio waliojaliwa,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

Syria yatungojea, kama hivi yanakua,
Polepole hutokea, raia kuhujumiwa,
Kwa vyombo kutumia, wakubwa tu kuwafaa,
Wahuni wakitawala, Syria iko njiani!

No comments: