Sunday, June 17, 2012

Ili fisadi kulinda


IPO nia, ipo njia, hawawezi niachia,
Mimi wanitegemea, ya kwao kujilindia,
Nani watamuachia, salama wakabakia ?
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Hamuwezi kuyajua, jinsi nilivyowanyanyua,
Hata watu kuibia, ili nchi kuchukua,
Miezi niliumia, kofia wapate vaa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Yamini tukajilia, awali wewe ingia,
Na wa pili nitakuwa, dhahiri kurudishiwa,
Kila nilichotumia, na ziada kupatiwa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Pembeni tulifagiwa, ili tohara kutia,
Wagomvi wakaambiwa, waache ya kuyazua,
Na timu zikaingia, ili langu ndilo kuwa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Dhahabu waliojaa, yapaswa kuongezewa,
Benki walopakuliwa, sahani kuongezewa,
Miradi waliopewa, yabidi kupanuliwa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Na tuliojijengea, ulinzi unatakiwa,
Ya kwetu tukajilia, bila ya kusumbuliwa,
Na mimi chaugo nawa, hata nyie mkikataa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Mihela sasa yajaa, kila kona twapakua,
Nasibu tumezizua, kila siku zaingia,
Tayari twajiandaa, siku itapoingia,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Sura yangu yasifiwa, waiona maridhia,
Kingine sikuumbiwa, ila rais nikuwa,
Na sasa ninasomea, masta ya ushujaa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Imani nitapindua, na mioyo kuitwaa,
Nisiate kutangia, vikoba vyao kujaa,
Kwa langu mie ikawa, chaguo lisilo waa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Ukubwa ni majaliwa, na udogo naridhia,
Ila ukiangalia, namna ninavyokaa,
Utaona ninapwaya, juu zaidi yafaa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Juu nilipopandia, teke ngazi nikatia,
Wengi wameninyanyua, chini nikawatupia,
Rahisi waliokuwa, ndio niliowafaa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Ya baba nilikataa, nikaona yakuzua,
Ninazidi kushupaaa, ukuu kukuakua,
Ibra kuchaguliwa, si ajabu Tanzania,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Labda akitokeya, madoa asiyekuwa,
Na hilo nitashangaa, kati yetu wajamaa,
Bepari tumeshakua, na madoa ni tabia,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!

Bepari tumeshakua, na madoa ni tabia,
Kama duma na madoa,  hawezi vingine kuwa,
Huyo ukijionea, ni marara atakuwa,
Ukubwa nitaupewa, ili fisadi kuhami!


No comments: