Tuesday, June 12, 2012

Watu ukiwaibia



NI mkono wenye haki, lake budi kutimia,
La shari haushiriki, wala heri kujapwaya,
Yake yote stahiki, daima inavyokuwa,
Watu ukiwaibia, wako nawe huibiwa !

Watu hawadhulumiki, kuna toa na kutwaa,
Ifanye hiyo mikiki, leo ukaambulia,
Wana mbali hawafiki, nao watadhulimiwa,
Watu ukiwaibia, wako nawe huibiwa !

Cha mtu hakiibiki, ukweli ninakwambia,
Uizi ukiafiki, kesho yako angalia,
Mjukuu hamiliki, hicho utakachokitwaa,
Watu ukiwaibia, wako nawe huibiwa !

Kwa urafiki au chuki, watu ukiwahadaa,
Deni mbali halivuki, wanao yatawatukia,
Wakutwe na wazandiki, lengo likawapotea,
Watu ukiwaibia, wako nawe huibiwa !

Kiumbe hadhulumiki, hili kaa ukijua,
Fanza wako unafiki, mabaya kumzulia,
Nawe mbali haufiki, hufikwa ukashangaa,
Watu ukiwaibia, wako nawe huibiwa !

kaipigeni miswaki, harufu kuziondoa,
Mambo yenu unafiki, hali ukweli mwaujua,
Lakini hadanganyiki, mkweli anayejua,

Maisha ni mamluki, kila mtu hununua,
Ya kheri ukiafiki, maovu hukuambaa,
Ubaya ukiashiki, balaa huzinunua,

Nisemayo sidhihaki, japo mnayatania,
Hadi ujapo mkuki, wa Ziraili kukwingia,
Ndipo utatahamaki, hivi kweli inakuwa,




No comments: