Kufilisika si kwema, kuwe kwa kila aina,
Ila ni kubwa nakama, ukiwa ni kwongozana,
Ikawa mwarudi nyuma, kwenda mbele mnaona,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !
Watu hukosa ujima, pasiwe nala kusana,
Mbingu zikawa zahama, na dhiki zawatafuna,
Pasiwe mwenye kusema, lililojaa maana,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !
Nchi ikiwa yatima, kwa viongozi haina,
Haina inachosema, wala kuweka amana,
Na haishi kuazima na wengine kukopana,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !
Hulemaa wakazama, viongozi wakanuna,
Pasiwe yenye adhima, wawezayo kuyafanya,
Lakini wanarindima, kwa kung'aa na kunona,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !
Ufukara huu ngoma, kuicheza patasuna,
Zinatoweka hekima, ikabakia kuguna,
Na busara huroroma, usingizini kutuna,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !
Akili huwa zagoma, hata vichwa ukikuuna,
Kisogo ukakitoma, na ukuta kugusana,
Giza likawa latoma, na kitu kutokiona,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !
Hubakia vicherema, vichuguu hutonena,
Pasi nuru ya kalima, vilimo kutoviona,
Wakaingia songoma, yao wakaja kuvuna,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !
Naye siye maamuma, ayajua maulana,
Hamuwezi pewa chema, msio na muamana,
Mtapewa chenu kima, hadi kuwa waungwana,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !
Monday, June 18, 2012
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment