Monday, June 18, 2012

Ufukara wa kutisha

Kufilisika si kwema, kuwe kwa kila aina,
Ila ni kubwa nakama, ukiwa ni kwongozana,
Ikawa mwarudi nyuma, kwenda mbele mnaona,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !

Watu hukosa ujima, pasiwe nala kusana,
Mbingu zikawa zahama,  na dhiki zawatafuna,
Pasiwe mwenye kusema, lililojaa maana,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !

Nchi ikiwa yatima, kwa viongozi haina,
Haina inachosema, wala kuweka amana,
Na haishi kuazima na wengine kukopana,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !

Hulemaa wakazama, viongozi wakanuna,
Pasiwe yenye adhima, wawezayo kuyafanya,
Lakini wanarindima, kwa kung'aa na kunona,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !

Ufukara huu ngoma, kuicheza patasuna,
Zinatoweka hekima, ikabakia kuguna,
Na busara huroroma, usingizini kutuna,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !

Akili huwa zagoma, hata vichwa ukikuuna,
Kisogo ukakitoma, na ukuta kugusana,
Giza likawa latoma, na kitu kutokiona,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !

Hubakia vicherema, vichuguu hutonena,
Pasi nuru ya kalima, vilimo kutoviona,
Wakaingia songoma, yao wakaja kuvuna,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !

Naye siye maamuma, ayajua maulana,
Hamuwezi pewa chema, msio na muamana,
Mtapewa chenu kima,  hadi kuwa waungwana,
Ufukara wa kutisha, ni ule wa uongozi !

No comments: