Monday, June 18, 2012

Aabuduye wageni



Aabuduye wageni, kwao wao si mgeni,
Na mkazi baniani, atamshinda mgeni,
Maisha kitu amini, ukaapo uthamini,
Aabuduye wageni, huwa hanayo mzizi !

Wengi wako mashakani, kwa kuthamini wageni,
Huipiga abautani, mambo mkija wahini,
Dhikini kuwaacheni, mkakosa tumaini,
Aabuduye wageni, huwa hanayo mzizi !

Watawaacha jangwani, hamna matumaini,
Wakarudi masikani, wakuitako nyumbani,
Hali yenu sasa duni, mmebaki makatuni,
Aabuduye wageni, huwa hanayo mzizi !

Huu ni wao uhuni, huufanza duniani,
Hawali nanyi amini, wala msiwaamini,
Ila kiasi hisani, mkawajua moyoni,
Aabuduye wageni, huwa hanayo mzizi !

Wengi wao ni rehani, na riba huwazaini,
Wakaufanza utani, yao mkayathamini,
Njia wakiibani, wakitoka hamuwaoni,
Aabuduye wageni, huwa hanayo mzizi !


No comments: