Thursday, June 28, 2012

Tuna haki ya kuiba



Chama chetu ni ruhusa, kuiba na kubakua,
Leseni tumeshapewa, nani ataka zuia,
Nchi nzima tumejaa, makaburi kuchimbua,
Tuna haki ya kuiba, wengine hawana haki !

Makaburi kuchimbua, haki za kuizikia,
Na usawa kukataa, sisi pekee tukawa,
Wajinga wawe waliwa, pasiwe wa kuulizia,
Tuna haki ya kuiba, wengine hawana haki !

Kibali tumeamua, wenyewe tunakitoa,
Nani atayekataa, na mpini twajishikia,
Makali tukiachia, wote nyie mtaumia,
Tuna haki ya kuiba, wengine hawana haki !

Kuiba tukiamua, saa yote twachukua,
Ni yetu yanshakuwa, serikali jina yawa,
Chama kimeshikilia, nani wa kukikosoa,
Tuna haki ya kuiba, wengine hawana haki !

Kudanganya ni tabia, yabidi kuendelea,
Wajinga Watanzania,c hama chetu kinajua,
Kijani ikiingia, na njano inafuatia,
Tuna haki ya kuiba, wengine hawana haki !

Kijani ikiingia, na njano hufuatia,
Wao basi hupagawa, yote wakatuachia,
Dawa yetu yawafaa, hawana wanalojua,
Tuna haki ya kuiba, wengine hawana haki !

Kuwapiga ni tabia, na maji kuwamwagiwa,
Pilipili yalojaa, nao wanafurahia,
Aklili zimewalegea, kitu gani wanajua ?
Tuna haki ya kuiba, wengine hawana haki !

No comments: