Monday, June 18, 2012

Mchezo wa kuigiza



Ukweli tukiujua, watu wema tungekuwa,
Ni mafupi yalokuwa, maisha kwenye dunia,
Siku kasi hupotea, na wewe ukapotea,
Maisha tunayoishi, mchezo wa kuigiza:
Tunapanda jukwaani,
Kwa muda ni wasanii,
Kisha chini tunashuka,
Na kupotelea mbali!

Ni mchezo ulokuwa, watu tunajichezea,
Makubwa 'kifikiria, kichwa bure waumia,
Muda hautakawia, watalishusha pazia,
Maisha tunayoishi, mchezo wa kuigiza:
Tunapanda jukwaani,
Kwa muda ni wasanii,
Kisha chini tunashuka,
Na kupotelea mbali!

Ukubwa huulilia, hadi ukajipatia,
Madudu ukaachia, watu wote kukuchukia,
Kisha hubaki walia, nafasi tena  kupewa,
Maisha tunayoishi, mchezo wa kuigiza:
Tunapanda jukwaani,
Kwa muda ni wasanii,
Kisha chini tunashuka,
Na kupotelea mbali!

Watu wanjisomea, shahada wakazitwaa,
Wengine bure wapewa, tena wanachekelea,
Kitu hawakutumia, na uchungu hawatojua,
Maisha tunayoishi, mchezo wa kuigiza:
Tunapanda jukwaani,
Kwa muda ni wasanii,
Kisha chini tunashuka,
Na kupotelea mbali!

Mwenye elimu huvia, na yake yakapwelea,
Pasiwe kusaidiwa, japo keshasaidia,
Na pembeni hutupiwa, kcihwani kujiozea,
Maisha tunayoishi, mchezo wa kuigiza:
Tunapanda jukwaani,
Kwa muda ni wasanii,
Kisha chini tunashuka,
Na kupotelea mbali!

Wazuri wanazaliwa, bahata wakachezea,
Wakija kujitambua, umri wakomalia,
Wakabaki jichubua, kumbe ndio wajiua,
Maisha tunayoishi, mchezo wa kuigiza:
Tunapanda jukwaani,
Kwa muda ni wasanii,
Kisha chini tunashuka,
Na kupotelea mbali!

Mamissi waliokuwa, uzee huja ingia,
Watu wakawakimbia, uzuri waliojaliwa,
Wengine wakaridhia, mapenzi kuyanunua,
Maisha tunayoishi, mchezo wa kuigiza:
Tunapanda jukwaani,
Kwa muda ni wasanii,
Kisha chini tunashuka,
Na kupotelea mbali!

Wachamungu huishiwa, watu wakawanunua,
Mfukoni kuwatia, yao wakakubalia,
Ghafla hushtukia, sakramauti yatua,
Maisha tunayoishi, mchezo wa kuigiza:
Tunapanda jukwaani,
Kwa muda ni wasanii,
Kisha chini tunashuka,
Na kupotelea mbali!

Nani atawaombea, waliokwishalaaniwa,
Kufuru waliotia, na Mola kumchezea,
Utani huwarudia, na shiriki kushtakiwa,
Maisha tunayoishi, mchezo wa kuigiza:
Tunapanda jukwaani,
Kwa muda ni wasanii,
Kisha chini tunashuka,
Na kupotelea mbali!

No comments: