Tuesday, June 12, 2012

Watu ukiwazulia



NI mkono wenye haki, lake budi kutimia,
La shari haushiriki, wala heri kujapwaya,
Yake yote stahiki, daima inavyokuwa,
Watu ukiwazulia, wako nao huzushiwa!

Watu hawadhulumiki, kuna toa na kutwaa,
Ifanye hiyo mikiki, leo ukaambulia,
Wana mbali hawafiki, nao watadhulimiwa,
Watu ukiwazulia, wako nao huzushiwa!

Cha mtu hakiibiki, ukweli ninakwambia,
Uizi ukiafiki, kesho yako angalia,
Mjukuu hamiliki, hicho utakachokitwaa,
Watu ukiwazulia, wako nao huzushiwa!

Kwa urafiki au chuki, watu ukiwahadaa,
Deni mbali halivuki, wanao yatawatukia,
Wakutwe na wazandiki, lengo likawapotea,
Watu ukiwazulia, wako nao huzushiwa!

Kiumbe hadhulumiki, hili kaa ukijua,
Fanza wako unafiki, mabaya kumzulia,
Nawe mbali haufiki, hufikwa ukashangaa,
Watu ukiwazulia, wako nao huzushiwa!
Watu ukiwazulia, wako nao huzushiwa!

kaipigeni miswaki, harufu kuziondoa,
Mambo yenu unafiki, hali ukweli mwaujua,
Lakini hadanganyiki, mkweli anayejua,
Watu ukiwazulia, wako nao huzushiwa!

Maisha ni mamluki, kila mtu hununua,
Ya kheri ukiafiki, maovu hukuambaa,
Ubaya ukiashiki, balaa huzinunua,
Watu ukiwazulia, wako nao huzushiwa!

Nisemayo sidhihaki, japo mnayatania,
Hadi ujapo mkuki, wa Ziraili kukwingia,
Ndipo utatahamaki, hivi kweli inakuwa,

No comments: