Monday, June 18, 2012

Alozoea kuomba



Kuomba aliyezoea, huwa ni yake tabia,
Vigumu kuiachia, hiyo nayo kazaliwa,
Nyayo anazifuatia, karunini kusishia,
Alozoea kuomba, tabia huendelea!

Hawezi vingine kuwa, hiyo ni yake tabia,
Kayajenga mazoea, kila kitu kutegemea,
Aibu wala si haya, kwake anayoijua,
Alozoea kuomba, tabia huendelea!

Kuomba ataringia, na wengine kuvutia,
Akaijenga himaya , yao watu wa kupewa,
Roho zote zikavia, kwa wengihe kutegemea,
Alozoea kuomba, tabia huendelea!

Mola hili achukia, viumbe mliojaliwa,
Viungo vikatimia, na akili kuzipewa,
Thamani huwapungua, muwe msiyemfaa,
Alozoea kuomba, tabia huendelea!

Viumbe mnatakiwa, jasho lenu kulitoa,
Mlacho kufurahia, kazi mmekifanzia,
Ila hayo ya kupewa, sivyo y anayotokea,
Alozoea kuomba, tabia huendelea!

Yaoneni ni kinyaa, muanze kuyakimbia,
Watu wakiwatumia, kwa  nguvu kuyakataa,
Msipokee dagaa, hali mwajua kuvua,
Alozoea kuomba, tabia huendelea!

No comments: