Thursday, June 14, 2012

Usiende na kababu



NAMI nieje bajia, ni nini cha kunisibu,
Kababu wamchukua, unaniacha naibu,
Na sote tumebukua, hadi huko Ughaibu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?

Ni chache zangu wakia, ila ni kitu  muhibu,
Wahindi hunililia, kwa kukosa uraibu,
Pilipili nikitiwa, wala siwi na ghadhabu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?

Mkate kashindiliwa, hana aibu kibabu,
Na nyama kahujumiwa, mla mboga hana jibu,
Na unga hajaujua, keshamuhini Mwajabu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?

Kababu kahifadhiwa, sura yake ya  ajabu,
Kwa moja hakutulia, sembuse kutaadibu,
Sura zote huchukua, nyingine bila hesabu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?

Bajia namshangaa, hana majibu ya ghibu,
Kila kitu akamia, na kumla nako taabu,
Pilipili akitiwa, utadhani mraibu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?

No comments: