Thursday, June 14, 2012
Usiende na kababu
NAMI nieje bajia, ni nini cha kunisibu,
Kababu wamchukua, unaniacha naibu,
Na sote tumebukua, hadi huko Ughaibu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?
Ni chache zangu wakia, ila ni kitu muhibu,
Wahindi hunililia, kwa kukosa uraibu,
Pilipili nikitiwa, wala siwi na ghadhabu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?
Mkate kashindiliwa, hana aibu kibabu,
Na nyama kahujumiwa, mla mboga hana jibu,
Na unga hajaujua, keshamuhini Mwajabu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?
Kababu kahifadhiwa, sura yake ya ajabu,
Kwa moja hakutulia, sembuse kutaadibu,
Sura zote huchukua, nyingine bila hesabu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?
Bajia namshangaa, hana majibu ya ghibu,
Kila kitu akamia, na kumla nako taabu,
Pilipili akitiwa, utadhani mraibu,
Usiende na kababu, nami nieje bajia ?
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment