Thursday, June 28, 2012

Mmea huu ng'oeni



MMEA huu ng'oeni, mtakuwa mashakani,
Mmea wa mumiani, na wauaji wa imani,
Haki wasioamini, na usawa wahaini,
Mmea huu ng'oeni, kabla haujakuwa!

Huwatumia afkani, walojaa kisirani,
Wakawaua amini, wabia wetu nchini,
Ya kwao kuwa yakini, ili wapande thamani,
Mmea huu ng'oeni, kabla haujakuwa!

Mungiki ni wahisani, wameingia nchini,
Wawafundisha uhuni, watu wa chama fulani,
Na wengine serikalini, nao pia wazaini,
Mmea huu ng'oeni, kabla haujakuwa!

Wanafikiri uhuni, waweza leta imani,
Na sheria za hisani, njiani wanabaini,
Haki zisizobaini, binadamu duniani,
Mmea huu ng'oeni, kabla haujakuwa!

Tutafika mahakamani, tuutete walakini,
Mabingwa wenye yakini, wakajaa kizimbani,
Wayaseme ya ubani, sio uongo nuksani,
Mmea huu ng'oeni, kabla haujakuwa!

Nchi hii mashkani, mageuzi tubaini,
Haufai usukani, udhaifu umewini,
Na nchi i mashakani, akibakia kitini,
Mmea huu ng'oeni, kabla haujakuwa!

No comments: