Monday, June 18, 2012

Mdharau watu wake



Huidharau mwenywe, mdharau watu wake,
Kiki'sha chake kiwewe, ni ukweli ufumbuke,
Mgeni ni kama mwewe, hutua chake adake,
Mdharau watu wake, hujidharau mwenywe.

Mgeni ni kama mwewe, hutua chake adake,
Kwa kasi yake atuwe, papo hapo aondoke,
Kwalo hilo muelewe, si udugu autake,
Mdharau watu wake, hujidharau mwenywe.

Kwalo hilo muelewe, si udugu autake,
Hutaka chake azowe, na nyumbani akiweke,
Vipi akufae wewe, yapungue mali yake ?
Mdharau watu wake, hujidharau mwenywe.

Vipi akufae wewe, yapungue mali yake ?
Mlishwao msiwe, wa pipi za mate yake,
Muone mbarikiwe, hatimaye mzuzuke,
Mdharau watu wake, hujidharau mwenywe.

Hujidharau mwenyewe, mdharau watu wake,
Huwasemi waelewe, kwalo hilo awajibike,
Hujidhania ngewe, naye siye ahusike,
Mdharau watu wake, hujidharau mwenywe.

Siyo hivyo nielewe, hayo si mashiko yake,
Kiongozi mwenye ndwele, huwalaumu wa kwake,
Akabakia mwenywe, nalo lake lisifanzike,
Mdharau watu wake, hujidharau mwenywe.

Hujidharau mwenyewe, mdharau watu wake,
Ni nani amuokowe, ikifika siku zake,
Huja yake yaishie, alipo asitukuke,
Mdharau watu wake, hujidharau mwenywe.

No comments: