Sunday, June 17, 2012

Cheo nimefinyangwa



Mrithi nimeambiwa, mwingine hawezi kuwa,
Nimefinyangwa radhia, na kiti nimewekewa,
Ni chaguoa la balaa, siku yangu nangojea,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Ni chaguo la nazaa, kwa cheo kukichukua,
Matapishi kuyazoa, chakula kikarejea,
Wala pasiwe kinyaa, watu wawe washangaa,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Ni chaguo la hidaya, na tunu kuzawadiwa,
Na vibwebwe vikatia, karamu kuandaliwa,
Na dini za butwaa, zisiache kuchangia,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Ni chaguo la makaa, majibu yalobakia,
Na masinzi kusingia, machoni wanja yakawa,
Na aibu na vihaya, vijae katika kaya,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Wenye njaa hununua, hata juu walokuwa,
Busara kuwapindua, uzuzu nikawatia,
Na hekima kuing'oa, maghofu yakabakia,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Sina ninayemhofia, ila kalamu ni baa,
Hasa zikijaujua, ukweli ninaojua,
Na nia kuzifukua, kuiuza Tanzania,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Udhalili nakataa, masimango yatazua,
Si wa kupambanua, na pepo kuangalia,
Na yazukapo mapya, siwezi kuyaezua,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Cheo nyumba ya hadaa, ni nani asiyejua ?
Roho njema si shujaa, yatakiwa roho mbaya,
Haya yangu majaliwa, ninaona ninafaa,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Watu ukiwapa raha, mimi huwa naumia,
Nawatakia balaa, tena wazidi umia,
Moyoni kwangu furaha, rahisi kuabudiwa,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Rahisi kuabudiwa, na ukubwa kuutwaa,
Kidogo ukitumia, bwerere kujivunia,
Hadi vyungu vikajaa, na mengine kubakia,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

Nna raha ya kuachiwa, moto kutokumbatiwa,
Na vijinga kuving'oa, na vikuni vya kutia,
Wakati ukifikia, nao moto ukapoa,
Cheo nimefinyangwa, ni mimi tu kuachiwa !

No comments: