Sunday, June 17, 2012

Dokta na doktori

 DOKTA ni wa kupewa, doktori kasomea,
Udokta ni hidaya, zawadi watu hupewa,
Hajui au ajua, ukuruba huliliwa,
Kumbe iko tofauti, dokta na doktori ?

Barua ukichukua, vyema ukaangalia,
Tarishi bora ukawa, katika yako dunia,
Hili utazawadiwa, dokta nawe ukawa,
Kumbe iko tofauti, dokta na doktori ?

Hata anayefagia, pasibakie udhia,
Kila kona ikang'aa. ma vizuri kunukia,
Huyo naye ni sawia, udokta akapewa,
Kumbe iko tofauti, dokta na doktori ?

Choo ukiangalia, usafi kutopungua,
Pasiwe nayo kinyaa, pia na harufu mbaya,
Dokta budi ukawa, watu tukakusifia,
Kumbe iko tofauti, dokta na doktori ?

Mganga uliyetimia, unajua kuagua,
Wagonjwa kuwatibia, afya ikarejea,
Udokta ukijaliwa, ni halali inakua,
Kumbe iko tofauti, dokta na doktori ?

Doktori hutokuwa, hadi kwenda kusomea,
Shahada nayo ukiwa, uzamili 'meingia,
Utafiti ukazua, na majibu kuyatoa,
Kumbe iko tofauti, dokta na doktori ?

Unatakiwa kubukua, na nukuu kuzitia,
Kichwa ukakisugua, hadi kipara kutia,
Halafu ukatetea, hicho ulichogundua,
Kumbe iko tofauti, dokta na doktori ?

Ubigwa utaridhiwa, kwa mengi sana kujua,
Eneo dogo  likawa, nje-ndani walijua,
Hata unaposinzia, majibu sahihi watoa,
Kumbe iko tofauti, dokta na doktori ?

Mlevi hautokuwa, ovyo kujiropokea,
Husema wanaojua, majibwa makali huwa,
Kuliko ya muangaliwa, ili kuficha kadhia,
Kumbe iko tofauti, dokta na doktori ?




No comments: