Tuesday, June 12, 2012

Watu ukiwadhulumu



NI mkono wenye haki, lake budi kutimia,
La shari haushiriki, wala heri kujapwaya,
Yake yote stahiki, daima inavyokuwa,
Watu ukiwadhulumu, wako watadhulumiwa !

Watu hawadhulumiki, kuna toa na kutwaa,
Ifanye hiyo mikiki, leo ukaambulia,
Wana mbali hawafiki, nao watadhulimiwa,
Watu ukiwadhulumu, wako watadhulumiwa !

Cha mtu hakiibiki, ukweli ninakwambia,
Uizi ukiafiki, kesho yako angalia,
Mjukuu hamiliki, hicho utakachokitwaa,
Watu ukiwadhulumu, wako watadhulumiwa !

Kwa urafiki au chuki, watu ukiwahadaa,
Deni mbali halivuki, wanao yatawatukia,
Wakutwe na wazandiki, lengo likawapotea,
Watu ukiwadhulumu, wako watadhulumiwa !

Kiumbe hadhulumiki, hili kaa ukijua,
Fanza wako unafiki, mabaya kumzulia,
Nawe mbali haufiki, hufikwa ukashangaa,
Watu ukiwadhulumu, wako watadhulumiwa !

kaipigeni miswaki, harufu kuziondoa,
Mambo yenu unafiki, hali ukweli mwaujua,
Lakini hadanganyiki, mkweli anayejua,
Watu ukiwadhulumu, wako watadhulumiwa !

Maisha ni mamluki, kila mtu hununua,
Ya kheri ukiafiki, maovu hukuambaa,
Ubaya ukiashiki, balaa huzinunua,
Watu ukiwadhulumu, wako watadhulumiwa !

Nisemayo sidhihaki, japo mnayatania,
Hadi ujapo mkuki, wa Ziraili kukwingia,
Ndipo utatahamaki, hivi kweli inakuwa,
Watu ukiwadhulumu, wako watadhulumiwa !

No comments: