Sunday, June 17, 2012

Una umuhimu gani kwangu ?


Hali yangu hujajua, wala kuniangalia,
Vipi itatokea, iwe nakutetemekea,
Itakuw ani ngekewa, vigumu kujipatia,
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Ni maiti anakuwa, yule asiyenifaa,
Dunia hujiendea, hata nsipomjua,
Yakawa yanayokuwa, si ajabu kuzizua,
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Nini umenifanzia, yako wewe kuyajua,
Lipi umelisikia, adhana na kukimiwa,
Moyo ukakushtua, na  kuniombea dua,
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Lini tonge umetia, ukawa waniwazia,
Mkononi kusalia, wasiwasi kukujaa,
Hadi ukanipigia, hali  kutaka kujua ?
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Kipi umenitendea, niwezacho jivunia,
Nisiache toa dua, mazuri kukuombea ?
Kitandani 'kiingia, shukrani nikatoa ?
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Lini umeangaliwa, wangu niliojaliwa,
Hata shauri kutoa, pasina kugharamia,
Ukaelekeza njia, yao nao kutimia ?
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Lini umehudhuria, kilio nilichofiwa,
Na ubani kuutoa, kwa siri kujifanzia,
Na sadaka kuitoa, machozi yakapungua?
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Siku gani ilikuwa, yako mimi kunifaa,
UKapungua ukiwa, kwa hisia za jamia,
Nami nikajiinamia, na hofu kuiondoa?
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Sababu sijaijua, muhimu kwangu ukawa,
Hebu niachie njia, uendako elekea,
Na shari ukiizua, kheri nitakuombea,
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Madeni wanilindukia, hayawezi kupungua,
Na riba zanizidia, nazidi kudidimia,
Huruma hukujaliwa, unafanya ya mzaha?
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Naona umelaaniwa, ya watu kutosikia,
Kaziyo kushtukia, ukazichora sanaa,
Na mengine ya umbeya, tija yasiyojaliwa,
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Viwanda umeviua, na ajira kupotea,
Vijana wakukataa, jahili unshakuwa,
Usiende kwenye mtaa, au utajaumia,
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Vijiji vimedumaa, huna aibu wala haya,
Wathubutu kujitoa, kujitia kidedea,
Ni maradhi umekuwa, budi tu kuvumiliwa,
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Kilimo kimejifia, na ubani hujatoa,
Watu wanakushangaa, matumizi wazidia,
Badhirifu umekuwa, fisadi wawaachia,
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Mikopo unayopewa, njiani inapotea,
Ukadai waibiwa, wezi hujatutajia,
Kidole chakuelekea, hivi hili hujajua ?
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Wapika na kupakua, msaada wakataa,
Na wasomi wamjeaa, uchumi wanaojua,
Wajifanza unajua, kumbe huna unalojua?
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?

Bajeti nakuambia, zuri kwako sijajua,
Ninazidi  kuumia, na watoto wasinyaa,
Nenda zako u balaa, wengine nawangojea,
Kama hunifanzii kitu, uweje muhimu kwangu?


tamathali ya bajeti 2012/2013

No comments: