Tuesday, June 12, 2012
Kila awaye mtusi
KWA mropoka matusi, hivi kweli anajua,
Kwa kila wake utusi, neno linamrejea,
Ama hiki kinamasi, wachache wanaojua,
Kila awaye mtusi, hujitukana wenyewe !
Kiumbe nje ya nafsi, roho moja tunakuwa,
Ukilitia kamasi, nalo lako linakuwa,
Na ukikipaka kinyesi, nawe kitakuenea,
Kila awaye mtusi, hujitukana wenyewe !
Ukiwa ni muflisi, waifilisi dunia,
Mtu kama wasiwasi, kiumbe ameumbiwa,
Nafsi ni ubinafsi, na utu ni majaliwa,
Kila awaye mtusi, hujitukana wenyewe !
Nafsi kama chunusi, kila mtu huchukua,
Si hodari kwa ususi, yake hayachi fumua,
Haijawa ni libasi, mwenyewe tu aijua,
Kila awaye mtusi, hujitukana wenyewe !
Za balaa na nuksi, ndivyo zinavyozaliwa,
Wengi wetu ni mijusi, na vikenge twazaliwa,
Hatuitoi nafasi, wengine wakajaliwa,
Kila awaye mtusi, hujitukana wenyewe !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment