Monday, June 18, 2012

Moja, mbili ya kichanga



NI ajabu ilokuwa, hii yetu Tanzania,
Hufa na kufufuliwa, za chama zilozokuwa,
Kale wakaifukia, na upya wakaanzia,
Serikali zetu hufa, na kisha zikafufuka:
Upya tena kuanza,
Moja, mbili ya kichanga !

Rojo sana imekuwa, serikali Tanzania,
Maji yanaizidia, siasa zilizojaa,
Na haliwi la kukua, lawama zaendelea,
Serikali zetu hufa, na kisha zikafufuka:
Upya tena kuanza,
Moja, mbili ya kichanga !

Kutengwa inatakiwa, ya serikali yakawa,
Chama mbali yake kuwa, utawala kuachia,
Vinginevyo kama yawa, mwisho watayajutia,
Serikali zetu hufa, na kisha zikafufuka:
Upya tena kuanza,
Moja, mbili ya kichanga !

Katikati huishia, kila linalobuniwa,
Rais mpya akawa, ya kale yasahauliwa,
Mapya akaanzia, na kichwa yasiyokuwa,
Serikali zetu hufa, na kisha zikafufuka:
Upya tena kuanza,
Moja, mbili ya kichanga !

Sanaa twajionea, sinema isiyofaa,
Kwa wengi kizaazaa, na nusura waijua,
Mambo yanavyojiendea, kama 'sukani watoa,
Serikali zetu hufa, na kisha zikafufuka:
Upya tena kuanza,
Moja, mbili ya kichanga !

Kama meli ingekuwa, kuzama ingeshakuwa,
Bali vizibo vyatiwa, tungali tunaelea,
Ukubwa ukilemaa, nchi nayo hulemaa,
Serikali zetu hufa, na kisha zikafufuka:
Upya tena kuanza,
Moja, mbili ya kichanga !

Hadhi juu ingekuwa, hii yetu Tanzania,
Nuksi tunajitia, kwa kujifanya tunajua,
Vilo bora twafumua, na ovyo kujishonea,
Serikali zetu hufa, na kisha zikafufuka:
Upya tena kuanza,
Moja, mbili ya kichanga !

Mikakati yatuumbua, kipi kipya kimekuwa,
Zama yaljaribiwa, na bado tukapotea,
Na mikono yaungua, jikoni tukiingia,
Serikali zetu hufa, na kisha zikafufuka:
Upya tena kuanza,
Moja, mbili ya kichanga !

Atunusuru Jalia, watuwe kutwangalia,
Uoza kuukimbia, kwa harufu na kinyaa,
Upya tukazaliwa, usafi 'kishadidia,
Serikali zetu hufa, na kisha zikafufuka:
Upya tena kuanza,
Moja, mbili ya kichanga !

No comments: