Thursday, June 28, 2012
Polisi bila digrii
Wasiyonayo digrii, upolisi hawafai,
Hawatajua jinai, na katiba kujiwahi,
Mamluki huwatii, sheria wasiitwii,
Polisi bila digrii, ni watumwa watakuwa !
La saba twawakinai, jeshi wanalikebehi,
Na dharau ya uhai, kwao yawa usanii,
Hakika hawatufai, kwa katiba hii rai,
Polisi bila digrii, ni watumwa watakuwa !
Washeheni wanoswii, tena kwa nyingi digrii,
Hawa tukiwastahi, jeshi litakuwa hai,
Siasa litakinai, ustadi wakawahi,
Polisi bila digrii, ni watumwa watakuwa !
Kusoma wasiojua, wakubwa wawatumia,
Kama maboi wakawa, hadi nyumbani kukaa,
Kila kitu wakapewa, wakubwa kuwafanyia,
Polisi bila digrii, ni watumwa watakuwa !
Ni maboi wanakuwa, majumbani kutumiwa,
Vijakazi nao pia, nyumbani kuwapikia,
Uoga ukawajaa, haki kutoitambua,
Polisi bila digrii, ni watumwa watakuwa !
Haki wanaoijua, mambo haya hukataa,
Yao wakayaamua, ya nchi yenye kufaa,
Na uongo kukataa, na watu kuwahofia,
Polisi bila digrii, ni watumwa watakuwa !
Akili hutumia, si ujinga kuuoa,
Daraja kujipandia, haki ikitambuliwa,
Na kisomo juu kuwa, ikawajua dunia,
Polisi bila digrii, ni watumwa watakuwa !
Mahakama zazuliwa, Ulaya kuangalia,
Watu wanaosumbua, kule watahukumiwa,
Nchi haitawatetea, wala wakuu walokuwa,
Polisi bila digrii, ni watumwa watakuwa !
Wenyewe mnatakiwa, vijana kuyakataa,
Wakubwa kutowatumia, watu kwenda kuwaua,
Dhambi mnaichukua, ni vipi mtajiokoa,
Polisi bila digrii, ni watumwa watakuwa !
Hamuwezi jiokoa, motoni mtaingia,
Unguja hili tambua, na nyie wa bara pia,
Ujinga ukiamriwa, huo lazima kukataa,
Polisi bila digrii, hivi leo hawafai !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment