Sunday, June 17, 2012

Mla vya ovyo hunuka



Hutoacha kumtambua, mla vya ovyo hunuka,
Katu haitatokea, uoza ukamtoka,
Hawezi akanukia, kunuka yake hulka,
Mla vya ovyo hunuka, hilo hawezi kimbia !

Asije kukaribia, roho ikajachafuka,
Sio wanaovutia, karibuwe wakifika,
Ndipo utawachukia, mkono kutowashika,
Mla vya ovyo hunuka, hilo hawezi kimbia !

Usafi wawaambaa, mioyo kuwacharuka,
Uchafu waufatia, na uoza wakashika,
Kisha wakatarajia, na watu kukubalika,
Mla vya ovyo hunuka, hilo hawezi kimbia !

Wanashindwa jitambua, ni bidhaa wauzika,
Bei ukiigundua, rahisi kununulika,
Si aghali nakwambia, milioni hutofika,
Mla vya ovyo hunuka, hilo hawezi kimbia !

Yao yote yanavia, si wa kutamanika,
Za mkato zao njia, chooni zinapofika,
Na harufu huchukua, hadi mbali ikafika,
Mla vya ovyo hunuka, hilo hawezi kimbia !

Maji wanayakimbia, na sabuni kutoshika,
Kila wakijichambia, mkononi vinashika,
Kila ukiwachungua, hauwezi malizika,
Mla vya ovyo hunuka, hilo hawezi kimbia !

Kalamu naiachia, mbali siwezi kufika,
Tohara naihofia, isije kumalizika,
Najisi ninaiambaa, isije kukanyagika,
Mla vya ovyo hunuka, hilo hawezi kimbia !

No comments: