Monday, June 18, 2012

Chama ana malaria ?

KAMA chama chaugua, hivi nini inakuwa,
Ugonjwa ukaujua, eti tena malaria,
Chandalua kimevaa, wapi mbu kaingia ?
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?

Kauli za kuugua, kila siku zatokea,
Huzuka kwenye mitaa. pia kwenye majukwaa,
Kichwani yameingia, yasemwayo hushangaa,
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?

Chama kinajitambua, uchama kikalilia,
Kisha huchanganyikiwa, uchama kikakataa,
Halafu kikakwambia, serikali kimekua,
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?

Huvaa hii kofia, mengi kikayaongea,
Na ilani zisokuwa, uchama kinachofaa,
Si kwa nchi kutumiwa, wala watu kuwafaa,
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?

Na mwili ukipungua, watu hukiangalia,
Mengine wakadhania, kukonda ilivyokuwa,
Hungong'ona nje wakiwa, eti kimeshaukwaa,
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?

Dawa kinapotumia, malaria kuondoa,
Afya hukirudia, ila akili nazaa,
Pia ungali umbeya, eti dawa zinakifaa,
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?

Ukimwi naukataa, jama haya malaria,
Kichwani yameingia, ndiyo tunayojionea,
Waganga hawataa, hospitali twatakiwa,
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?

Chama anaugulia, huku na huku ahaha,
Ugonjwa hajaujua, kulogwa anahofia,
Huyu ni wetu jamaa, ukweli sikumwambia ?
Chama kina malaria, au huu ni ukimwi ?

Kumuuguza inafaa, presha ikapungua,
Amana tumeachiwa, lazima kumwangalia,
Akija kutufilia, sisi tutalaumiwa,
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?

Kichwani inapokaa, mbaya kweli malaria,
Mtu huwa kama kichaa, vituko akavizua,
Njiani akakimbia, ikawa kubwa balaa,
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?

Yatakiwa kumzuia, asigongwe na motokaa,
Hadharani kujifia, watu wanamwangalia,
Huruma imeshapotea, watu weza jipitia,
Chama ana malaria, au huu ni ukimwi ?


No comments: