Thursday, June 14, 2012

Banda langu la udongo



LA udongo banda langu,  ukibomoa najenga,
Haiishi siku yangu, upya nitalipanga,
Wala sio hofu yangu, tetemeko likigonga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?

Ni tulivu moya wangu, utadhani ninaringa,
Supa ufakiri wangu, kwa mtu sijajigonga,
Na waridhi ua langu, weupe  lililoviringa,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?

Yapeta mapenzi yangu, yafanzika kwenye changa,
Wasiwe saizi yangu, kwenye ghorofa kutinga,
Maisha ni raha yangu, ukiwa haujanizonga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?

Dagaa chakula changu, lishe yake kama manga,
Mchuzi wangu wa dengu, na wali ninauchonga,
Kahawa yangu ya kungu, mato yangu kuyakinga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?

Ni tamu hisia zangu, hakuna anayepinga,
Wajua utamu wangu, hautoki kwa mganga,
Hawa ni asili yangu, kurogwa nimejikinga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?

Haya ni maisha yangu, wataka nini kulonga,
Haujui moya wangu, na lipi nililopanga,
Hiyo ndugu siri yangu, kwako katu ha'totinga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?

No comments: