Thursday, June 14, 2012
Banda langu la udongo
LA udongo banda langu, ukibomoa najenga,
Haiishi siku yangu, upya nitalipanga,
Wala sio hofu yangu, tetemeko likigonga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?
Ni tulivu moya wangu, utadhani ninaringa,
Supa ufakiri wangu, kwa mtu sijajigonga,
Na waridhi ua langu, weupe lililoviringa,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?
Yapeta mapenzi yangu, yafanzika kwenye changa,
Wasiwe saizi yangu, kwenye ghorofa kutinga,
Maisha ni raha yangu, ukiwa haujanizonga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?
Dagaa chakula changu, lishe yake kama manga,
Mchuzi wangu wa dengu, na wali ninauchonga,
Kahawa yangu ya kungu, mato yangu kuyakinga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?
Ni tamu hisia zangu, hakuna anayepinga,
Wajua utamu wangu, hautoki kwa mganga,
Hawa ni asili yangu, kurogwa nimejikinga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?
Haya ni maisha yangu, wataka nini kulonga,
Haujui moya wangu, na lipi nililopanga,
Hiyo ndugu siri yangu, kwako katu ha'totinga,
Banda langu la udongo, nilihofu tetemeko ?
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment