Tuesday, June 12, 2012
Hivi sasa wanachama
KAMA hili la hakika, inafaa kutazama,
Naambiwa imefika, zamu yao maamuma,
Wasiopo kuyashika, ya wengine kutazama,
Hata teja na vibaka, hivi sasa wanachama !
Uhakiki wapituka, zikazagaa tuhuma,
Wahesabika vibaka, hivi sasa wanachma,
Msajili hajataka, mmoja'moja kutazama,
Hata teja na vibaka, hivi sasa wanachama !
Hatunao uhakika, ya kusuka na kufuma,
Hivi nchi watashika, watu wanaororoma,
Na matusi kutapika, kama hii si nakama ?
Hata teja na vibaka, hivi sasa wanachama !
Chama kikastahika, wasafi budi kugema,
Hali isijechafuka, ukakuta unazama,
Magenge yaje kuzuka, ya rabsha na zahama,
Hata teja na vibaka, hivi sasa wanachama !
Budi kustaarabika, muungwana mwanachma,
Heshima akaiweka, mtu anapomtazama,
Akajua kwa hakika, hawa wetu wenye mema,
Hata teja na vibaka, hivi sasa wanachama !
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment